Raia wa Uingereza atekwa nchini Malawi
Polisi nchini Malawi wanaendelea na uchunguzi wa tukio la kutekwa nyara kwa raia wa Uingereza katika mji wa Blantyre, kitovu cha biashara cha nchi hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa ya polisi, Nusrat Osman, mwenye umri wa miaka 47, alitekwa na watu wanne majira ya mchana siku ya Ijumaa. Inadaiwa kuwa watekaji hao walikuwa wakitumia gari la rangi ya kijivu aina ya Nissan Dualis.
Mamlaka zimeahidi kutoa zawadi ya zaidi ya dola 17,000 za Marekani (takriban pauni 12,600) kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa za kuaminika zitakazosaidia kupatikana kwa Osman na kuwafikisha wahusika wa tukio hilo mbele ya sheria.
Osman, ambaye ni mama wa watoto wawili wadogo, anaripotiwa kufanya kazi katika kampuni ya ukaguzi wa hesabu nchini Malawi.
Vyombo vya habari vya nchini humo vimeripoti kuwa mume wake ameeleza hofu na majonzi makubwa kufuatia kutoweka kwake.
"Sijui alipo wala hali yake ikoje. Mke wangu ni mkaguzi wa hesabu na sina ugomvi na mtu yeyote," alinukuliwa akisema na gazeti la Nyasa Times.
Polisi wamesema hadi sasa chanzo cha utekaji huo hakijafahamika. Pia wameeleza kuwa watekaji bado hawajawasiliana na familia ya Osman wala mamlaka za serikali.
Wakati huo huo, Wizara ya Mambo ya Nje ya Uingereza imesema inafahamu taarifa za kutekwa kwa raia wake nchini Malawi na inaendelea kushirikiana kwa karibu na mamlaka za Malawi katika kufuatilia tukio hilo.