Moja kwa moja, Tunasitisha mashambulizi dhidi ya Israel, lakini tutaanza tena iwapo Israel itaishambulia Lebanon - Iran

Israel ilifanya mashambulizi ya anga dhidi ya Iran baada ya Tehran kuanza kurusha makombora kuelekea Israel siku ya Jumapili. Awali Donald Trump alizitaka nchi zote mbili "kusitisha mapigano".

Muhtasari

Skip Video and continue reading
  • s
  • a
  • Sonko
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • Dangote
  • xx
  • Lydia Wanjiku

Moja kwa moja

Na Lizzy Masinga & Asha Juma

  1. Tunasitisha mashambulizi dhidi ya Israel, lakini tutaanza tena iwapo Israel itaishambulia Lebanon - Iran

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Makao makuu ya jeshi la Iran Khatam al-Anbiya yamesema katika taarifa kwamba "tunasitisha shughuli za vikosi vya kijeshi".

    Lakini wameonya katika taarifa hiyo hiyo kwamba ikiwa mashambulizi yataendelea, "ikiwa ni pamoja na kusini mwa Lebanon," Iran itajibu "kwa nguvu zaidi kuliko hapo awali".

    Iran ilianza operesheni zake jana kujibu mashambulizi ya Israel kusini mwa Beirut. Israel ililipiza kisasi kwa kushambulia Iran.

    Maafisa waandamizi wa kisiasa na kijeshi wa Iran walikuwa wametoa maonyo jana jioni kwamba Iran ingejibu kijeshi kwa kile walichokielezea kama ukiukaji wa makubaliano ya kusitisha mapigano.

    Iran imesisitiza kwamba wanachukulia usitishaji mapigano nchini Lebanon kama sehemu ya usitishaji mapigano na Iran vile vile.

    Israel na Iran zinatafuta kusitisha mapigano mara moja - Trump

    Awali, Rais wa Marekani Donald Trump alisema mazungumzo ya mwisho kuhusu "amani" yanaendelea lakini "yanakabiliwa na ujinga au upumbavu ndani yake".

    Alisema katika chapisho lake kwenye mtandao wa Truth Social: "Pande zote mbili, Israeli na Iran, zinatafuta kufanya makubaliano ya haraka ya KUSITISHA MAPIGANO!"

    "Vikwazo vitasalia, kwa ukamilifu na athari zake, hadi 'Makubaliano ya Mwisho' yatakapofikiwa. Mambo yanatakiwa kufanyika kwa haraka," aliongeza.

    Soma zaidi:

  2. Mkuu wa WHO atembelea Uganda huku mlipuko wa Ebola ukienea kutoka DR Congo

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Dk Tedros Adhanom Ghebreyesus amewasili Uganda huku mamlaka ikiongeza juhudi za kudhibiti mlipuko wa Ebola unaohusishwa na nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).

    Uganda imethibitisha visa vinavyohusishwa na maambukizi ya kuvuka mpaka, huku maafisa wa afya wakiimarisha ufuatiliaji kwenye mpaka wake wa magharibi.

    Aliongeza kuwa mifumo ya afya ya Uganda inafanya kazi kwa ufanisi katika maeneo muhimu ya kudhibiti milipuko.

    Wakati wa ziara yake, Dkt Tedros alisifu mwitikio wa nchi, akisema Uganda imechukua "hatua za haraka na zenye uwezo mkubwa" kwa mlipuko huo, akiangazia jukumu la uchunguzi wa mpaka katika kubaini maambukizi kutoka nchi ya DRC.

    Kati ya maambukizi19 yaliothibitishwa nchini Uganda hadi sasa, 14 yanahusisha watu walioingia kutoka DRC, wakati watano ni raia wa Uganda. Vifo viwili vimerekodiwa kati ya wale waliovuka mpaka.

    "Tuko pamoja na familia zao kipindi hiki kigumu," Dk Tedros alisema, akiongeza kuwa WHO inaunga mkono Uganda pamoja na Vituo vya Afrika vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC) na washirika wengine wa kikanda.

    "Kwa ushirikiano unaoendelea, nina imani janga hili linaweza kudhibitiwa," alisema.

    Hali nchini Uganda inafungamana kwa karibu na mlipuko unaoendelea mashariki mwa DRC, ambao kufikia sasa umeingia wiki yake ya nne.

    Mamlaka za afya huko zilisema watu 12 wamepona ugonjwa wa Ebola wa Bundibugyo, wakati wagonjwa 283 bado, ama wametengwa au wanapokea matibabu katika maeneo 25 ya afya katika majimbo ya Ituri, Kivu Kaskazini na Kivu Kusini.

    Upimaji wa maabara umethibitisha sampuli chanya 515 tangu mlipuko huo ulipotangazwa, na vifo 91 vimerekodiwa.

    Jitihada za kuzuia kusambaa kwa ugonjwa huo zimekumbwa na changamoto za ukosefu wa usalama na upatikanaji wa vifaa katika maeneo ya mashariki mwa Congo, ambapo makundi yenye silaha yanaendeleza shughuli zake na kufikia baadhi ya maeneo ya vituo vya afya ni changamoto.

    Soma zaidi:

  3. Jaji Mkuu wa zamani Kenya akamatwa katika maandamano ya kupinga kuhamishwa kwa Hifadhi ya Wanyama pori

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Aliyekuwa Jaji Mkuu nchini Kenya amekamatwa katika maandamano ya kupinga mradi unaopendekeza uendelezaji wa miundombinu ndani ya Mbuga ya Kitaifa ya Nairobi.

    David Maraga alikuwa miongoni mwa wanaharakati kadhaa wa mazingira waliokamatwa Jumatatu asubuhi katika mji mkuu, Nairobi.

    Vikundi vya uhifadhi na wanaharakati walikuwa wamekusanyika kupinga mradi wa Huduma ya Wanyamapori ya Kenya kutenga sehemu ya mbuga hiyo kwa maendeleo ya miundombinu.

    Waandamanaji wanahoji kuwa mradi huo unaweza kutishia ardhi ya hifadhi na kuwa mwanzo wa kufanyika kwa miradi zaidi ya ujenzi ndani ya mbuga hiyo.

    Jaji Mkuu huyo wa zamani na anayewania urais amekuwa akizungumza kuhusu ulinzi wa mazingira.

    Waandamanaji wanadai takriban ekari 76 za makazi yaliyohifadhiwa zinaweza kuathiriwa na miradi ya miundombinu.

    Picha zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii zinaonyesha polisi wakiwatawanya waandamanaji kabla ya kuwazuilia Maraga na wanaharakati wengine.

    Kulingana na ripoti za vyombo vya habari vya ndani, Maraga na waandamanaji wengine kwa sasa wanazuiliwa katika Kituo cha Polisi cha Langa'ta.

    Shirika la Huduma la Wanyamapori nchini Kenya linakanusha madai ya unyakuzi wa ardhi, likisema mradi huo unahusisha kuhamisha na kuboresha Hifadhi hiyo ya Wanyama ya Nairobi ili kuboresha ustawi wa wanyama na huduma za uhifadhi.

  4. UN yahimiza Taliban kukomesha kukamatwa kwa wanawake juu ya sheria za mavazi

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan umeelezea wasiwasi kuhusu kukamatwa na kuwekwa kizuizini kwa wanawake katika jimbo la magharibi kwa madai ya kushindwa kufuata "kanuni za mavazi" na kuwasihi mamlaka ya Taliban kuwatendea watu wote sawa.

    Ujumbe wa Usaidizi wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan (UNAMA) haukubainisha ni wanawake wangapi wameathiriwa, ingawa vyombo vya habari vya ndani viliripoti wiki iliyopita kwamba takriban wanawake na wasichana 21 walikamatwa katika jimbo la Herat.

    Taliban wa Afghanistan hawakujibu ombi la Reuters la kutoa maoni.

    "UNAMA ina wasiwasi kuhusu kukamatwa na kuwekwa kizuizini mara nyingi kwa wanawake huko Herat...kwa madai ya kutofuata kanuni ya mavazi, jambo ambalo linazua wasiwasi mkubwa wa haki za binadamu," UNAMA ilisema katika chapisho kwenye mtandao wa X jioni ya Jumapili.

    "Tunawakumbusha mamlaka kwamba watu wote wana haki ya uhuru wa kutembea na kwamba watu wote, wanawake na wanaume, wana haki ya usawa mbele ya sheria," ilisema.

    Kukamatwa huko kunafuatia agizo la Taliban lililotolewa wiki iliyopita likiwakataza wanawake kuonekana hadharani bila kile ambacho mamlaka ilikielezea kama "hijab stahiki," kulingana na vyombo vya habari vya ndani.

    Ripoti zilisema agizo hilo lilionya kwamba wanawake ambao walishindwa kufuata kanuni za mavazi — ikiwa ni pamoja na wale wanaoonyesha nyuso zao au wanaojipodoa — watakabiliwa na adhabu. Reuters haikuweza kuthibitisha kwa uhuru agizo hilo.

    Tangu walipochukua madaraka huko Kabul mnamo 2021, Taliban imeweka vikwazo vikubwa kwa wanawake na wasichana katika nchi iliyoharibiwa na vita, ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa elimu, ajira na michezo, na kusababisha ukosoaji mkubwa wa kimataifa.

    Ripoti ya ⁠UNICEF iliyotolewa mwezi Aprili ilikuwa imeonya kwamba nchi hiyo iko katika hatari ya kupoteza zaidi ya walimu na wafanyakazi wa afya wa kike 25,000 ifikapo mwaka wa 2030 ikiwa vikwazo dhidi ya elimu ya wasichana na ajira kwa wanawake vitasalia kuwepo.

    Taliban inasema inaheshimu haki za wanawake kulingana na tafsiri yake ya sheria ya Kiislamu.

    Pia unaweza kusoma:

  5. Je mahakama kumsafisha Rigathi Gachagua?

    Gachagua

    Chanzo cha picha, EPA

    Na Laillah Mohammed

    BBC Swahili, Nairobi

    Jumatatu Juni 8 ni siku muhimu kwa aliyekuwa Naibu Rais wa Kenya Rigathi Gachagua almaarufu Riggy G, huku Mahakama Kuu ikitarajiwa kutoa uamuzi kuhusu iwapo kuondolewa kwake madarakani kupitia kura ya kutokuwa na imani naye, kulifuata katiba ya Kenya au la.

    Majaji Eric Ogolla, Anthony Mrima na Fred Mugambi watatoa uamuzi baada ya miezi kadhaa ya kusikiliza kesi hiyo yenye mvutano mkubwa wa kisiasa nchini Kenya.

    Gachagua aliondolewa rasmi madarakani Oktoba 17 mwaka 2024, baada ya bunge la taifa kupiga kura ya kumuondoa kwa zaidi ya wabunge 280 kuunga mkono hoja hiyo, kabla Seneti nayo kuidhinisha hatua hiyo.

    Alikabiliwa na mashtaka matano makuu yakiwemo ukiukaji wa katiba, matumizi mabaya ya ofisi, ufisadi, utakatishaji fedha, utovu wa nidhamu kazini na kuendesha siasa za ukabila.

    Miongoni mwa kauli zilizozua mjadala mkubwa ni ile aliyosema kuwa “wadau waliopiga kura ndio watanufaika zaidi serikalini,” kauli ambayo wakosoaji wake waliitafsiri kuwa serikali ya Kenya Kwanza ilikuwa ikibagua maeneo ambayo hayakumpigia kura Rais William Ruto.

    Katika kesi yake, Gachagua amedai kuwa kuondolewa kwake madarakani kulikuwa mpango wa kisiasa uliopangwa baada ya uhusiano wake na Rais Ruto kuzorota ndani ya serikali ya Kenya Kwanza.

    Pia aliiambia mahakama kuwa Bunge la Taifa na Seneti hazikumpa nafasi yakutosha kujitetea, akisema siku mbili pekee za kujiandaa zilikuwa chache mno kwa kesi nzito kama hiyo.

    Aidha, mawakili wake waliiambia mahakama kwamba Seneti iliendelea na kesi hiyo hata baada ya Gachagua kulazwa hospitalini, huku Spika wa Seneti Amason Kingi akikataa ombi la kuahirisha vikao hadi.

    Uamuzi wa leo unaweza kubadilisha kabisa siasa za Kenya kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

    Kama mahakama itakubaliana na Riggy G basi kiongozi huyo wa chama cha DCP atakuwa na nafasi ya kuwania tena uongozi katika uchaguzi mkuu mwakani.

    Lakini Ikiwa mahakama itatupilia mbali ombi la Gashagua, basi atabakia kuwa ‘King Maker’ kwani sheria za uchaguzi hazimruhusu kiongozi aliyeondolewa madarakani kupitia ‘Impeachment’ kuwania tena kiti cha uongozi au iwapo tu wakati wa uchaguzi awe bado mahakamani na hajafikia mahakama ya upeo.

    Je, mahakama itabatilisha kura ya kutokuwa na imani na Rigathi Gachagua au itaacha uamuzi wa Bunge na Seneti usimame?

    Unaweza kusoma;

  6. Rais wa Afrika Kusini atangaza msako mkali dhidi ya wahamiaji haramu

    Wageni hawa, ambao walikuwa wakitazama hotuba hiyo kwenye simu zao, wamepiga kambi nje ya ofisi ya Idara ya Mambo ya Ndani ya Durban wakisema wana hofu kwa maisha yao.

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa amehutubia taifa na kutangaza hatua kadhaa mpya za kukabiliana na uhamiaji haramu, wakati mvutano ukiongezeka kutokana na maandamano ya kupinga wageni na malalamiko kuhusu ukosefu mkubwa wa ajira.

    Hatua hizo ni pamoja na kuwafunga jela waajiri wanaowaajiri wafanyakazi wasio na vibali halali, kuanzisha mahakama maalum ili kuharakisha uhamisho wa wahamiaji wasio na vibali, na pia kuweka rejesta yenye taarifa za kibaiometriki “kwa kila mtu nchini” ili kuzuia wizi wa utambulisho.

    Hata hivyo, pia alionya wananchi wa Afrika Kusini wasijichukulie sheria mikononi mwao.

    Katika wiki chache zilizopita, mataifa kadhaa ya Afrika yamekuwa yakiratibu uhamisho wa baadhi ya raia wao kutokana na hofu ya vurugu kuongezeka.

    Makundi yanayopinga wahamiaji yanataka wahamiaji wasio na nyaraka kuondoka nchini na yameweka tarehe ya mwisho kuwa 30 Juni.

    Wiki iliyopita, mamia ya wahamiaji wa Kiafrika walikimbia makazi yao katika eneo la Overberg, Mkoa wa Western Cape, baada ya taarifa za vitisho vya nyumba kwa nyumba, pamoja na vifo vya raia wawili wa Msumbiji huko Mossel Bay.

    Wengi walikimbilia katika kumbi za jamii, ufukweni au milimani. Baadhi wameamua kurudi makwao, na mwishoni mwa wiki kundi jingine la takribani watu 140 lilipanda mabasi kwenda Malawi na Msumbiji.

    Mjini Durban, wageni wamekuwa wakipiga kambi nje ya ofisi ya Wizara ya mambo ya ndani kwa wiki kadhaa, wakisema wana hofu ya maisha yao.

    Unaweza kusoma;

  7. Maandamano yafanyika Tehran

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Tunapata baadhi ya picha sasa za maandamano yanayoiunga mkono serikali yanayoendelea Tehran, kufuatia mashambulizi ya Israel kwenye viunga vya kusini mwa Beirut.

    Wengi wa waandamanaji kwenye picha wamebeba bendera za Iran na Hezbollah, kundi la kisiasa na kijeshi linaloungwa mkono na Iran nchini Lebanon.

    .

    Chanzo cha picha, AFP

    .

    Chanzo cha picha, AFP

  8. Bei ya mafuta yapanda baada ya Iran kurusha makombora dhidi ya Israel

    .

    Chanzo cha picha, Anadolu via Getty Images

    Bei ya mafuta imepanda Jumatatu asubuhi barani Asia baada ya Iran kurusha makombora dhidi ya Israel kwa mara ya kwanza tangu kufikiwa kwa makubaliano ya usitishaji vita kati ya nchi hizo na Marekani mwezi Aprili.

    Bei ya kimataifa ya mafuta ghafi ilipanda kwa 2.6% hadi $95.50 (£71.60) kwa pipa, wakati mafuta yasiyosafishwa ya Marekani yalipanda kwa 2.5% hadi $92.75.

    Bei za nishati zimekuwa na mabadiliko makubwa tangu makubaliano ya kusitisha mapigano Aprili yalipokubaliwa.

    Bei zimepanda kwa karibu $95 katika wiki iliyopita huku wafanyabiashara wakipima athari za muda mrefu za vita dhidi ya mtiririko wa nishati duniani.

  9. Ripoti za vifo na majeruhi kutokana na tetemeko Ufilipino bado zinathibitishwa

    Uharibifu

    Chanzo cha picha, Philippine Red Cross

    Kumekuwa na ripoti za vifo kutokana na tetemeko Ufilipino, ingawa bado hazijathibitishwa rasmi.

    Mamlaka zinaendelea kuthibitisha takribanivifo vitano vilivyoripotiwa, kulingana na shirika la habari Reuters.

    Afisa mmoja wa polisi ameiambia AFP kwamba mtu mmoja amethibitishwa kufariki na wengine wanne wamejeruhiwa.

    Diego Mariano, afisa wa taarifa kutoka wakala wa kitaifa wa majanga wa Ufilipino, amesema kuwa ripoti za vifo na majeruhi zinafuatiliwa kwa karibu.

    Pia kuna taarifa za uharibifu mkubwa katika miundombinu mbalimbali.

    Ameonya wananchi kuepuka kurudi ndani ya nyumba zao au majengo mengine, hasa yale yanayoonesha dalili za uharibifu.

    Unaweza kusoma;

  10. Trump asema Netanyahu hatakuwa na jinsi, isipokuwa kukubali yatakayoafikiwa

    Trump

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Trump amesema kwamba Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu “hatakuwa na chaguo lingine” isipokuwa kukubali makubaliano yoyote ambayo Marekani itafikia na Iran.

    Akizungumza na Financial Times kupitia simu, Trump alisema: “Yeye hatakuwa na jinsi. Mimi ndiye ninayeamua. Mimi ndiye ninayeamua kila kitu. Yeye (Netanyahu) si anayeamua.”

    Trump pia aliiambia Axios hapo awali kwamba atamuomba Netanyahu asiendelee kulipiza kisasi dhidi ya Iran baada ya mashambulizi ya hivi karibuni, ili kuhakikisha pande hizo tatu zinaweza kufikia makubaliano.

    Kwa mujibu wa Financial Times, Trump alisema mashambulizi ya hivi karibuni hayajabadilisha chochote kuhusu mchakato wa makubaliano.

    “Tutaona jinsi itakavyomalizika,” alisema Trump.

    Unaweza kusoma;

  11. Tetemeko kubwa la ardhi limekumba eneo la kusini mwa Ufilipino

    Tetemeko

    Chanzo cha picha, Philippine Institute of Volcanology and Seismology

    Tetemeko kubwa la ardhi limetokea kusini mwa Ufilipino saa majira ya saa moja na dk 37 kwa saa za eneo hilo.

    Kwa sasa ukubwa halisi na kina cha tetemeko hilo bado havijathibitishwa kikamilifu.

    Kulingana na Taasisi ya Ufilipino ya Volkeno na Matetemeko ya Ardhi (Phivolcs), tetemeko hilo lilikuwa na ukubwa wa 7.0 na kina cha kilomita 10 (maili 6.2).

    Hata hivyo, Shirika la Utafiti wa Jiolojia la Marekani (USGS) limeripoti ukubwa wa 7.8 na kina cha kilomita 35, huku Kituo cha Utafiti wa Jiolojia cha Ujerumani kikiripoti ukubwa wa 7.8 na kina cha kilomita 50.

    Nchi kadhaa za eneo hilo, zikiwemo Ufilipino, Indonesia na Japani, zimetangaza tahadhari za tsunami.

    Unaweza kusoma;

  12. Israel imesema imefanya mashambulizi ya anga yaliyolenga maeneo ya magharibi na katikati ya Iran

    Moshi mzito

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Israel imesema imefanya mashambulizi dhidi ya maeneo ya magharibi na katikati ya Iran.

    “Dakika chache zilizopita, Jeshi la Anga la Israel lilishambulia maeneo ya kijeshi yanayomilikiwa na utawala wa kigaidi wa Iran katika maeneo ya magharibi na katikati ya Iran,” Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) limesema kupitia Telegram.

    Hakukuwa na maelezo zaidi yaliyotolewa kuhusu idadi ya walioumia au waliouawa, wala maeneo halisi yaliyolengwa katika mashambulizi.

    Katika hatua nyingine, Televisheni ya taifa ya Iran sasa inaripoti milipuko katika miji mitatu baada ya Israel kusema jeshi lake la anga limefanya mashambulizi dhidi ya maeneo ya kijeshi katikati na magharibi mwa Iran.

    “Milipuko kadhaa imeonekana kusikika Tehran, Tabriz na Isfahan,” televisheni ya taifa imeandika kupitia Telegram.

    Milipuko pia imeripotiwa kusikika karibu na mji wa kati wa Karaj.

    Taarifa hizi zinakuja wakati hali ya tahadhari ikiendelea kuongezeka kutokana na mfululizo wa mashambulizi kati ya Israel na Iran, huku maelezo zaidi yakitarajiwa kutolewa.

    Unaweza kusoma;

  13. Habari za asubuhi, karibu katika taarifa zetu.