'Marekani yadanganya kuhusu gharama za vita vya Iran' - Araqchi

Chanzo cha picha, TANSIM
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araqchi amesema Idara ya Ulinzi ya Marekani inatoa taarifa za uongo kuhusu gharama halisi za vita dhidi ya Iran.
Kauli hiyo inajiri baada ya Waziri wa Ulinzi wa Marekani Pete Hegseth kusema kuwa Marekani imetumia takriban dola bilioni 25 katika vita hivyo.
Akijibu madai hayo kupitia ukurasa wake wa mtandao wa X, Araqchi amesema Pentagon inadanganya, akidai kuwa hatua ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu imeigharimu Marekani dola bilioni 100 hadi sasa, kiasi ambacho ni mara nne zaidi ya kilichotajwa rasmi.
Araqchi ameongeza kuwa gharama zisizo za moja kwa moja kwa walipa kodi wa Marekani ni kubwa zaidi, akisema gharama ya kila mwezi kwa kila familia ya Marekani inakaribia dola 500 na inaendelea kuongezeka kwa kasi.
Amesema sera ya “Israel kwanza” inaifanya Marekani kuwa ya mwisho.
Kauli hiyo inakuja wakati Waziri wa Ulinzi wa Marekani Pete Hegseth akitetea matumizi ya vita dhidi ya Iran mbele ya Kamati ya Huduma za Kijeshi ya Baraza la Wawakilishi.
Hegseth amesema gharama ya vita hivyo hadi sasa inakadiriwa kuwa dola bilioni 25, akisisitiza kuwa matumizi hayo yalikuwa ya lazima kuizuia Iran kupata silaha za nyuklia.
Soma zaidi:









