Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Marekani kusaidia meli zilizokwama Hormuz - Trump

Inaelezwa kuwa ndege 100 na wanajeshi karibu 15,000 watahusika kwenye operesheni hiyo ambayo Rais huyo wa Marekani ameielezea kama “msaada wa kibinadamu” kwa mataifa yasiyohusika moja kwa moja na vita kati ya Marekani, Israel na Iran.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Yusuph Mazimu

  1. WHO yathibitisha mlipuko wa Hantavirus duniani, waua watatu kwenye meli ya kitalii

    Watu watatu wamefariki dunia kufuatia mlipuko unaoshukiwa kuwa wa virusi vya Hantavirus kwenye meli ya kitalii iliyokuwa safarini kutoka Argentina kuelekea Cape Verde, kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO).

    Mwanaume mmoja mwenye umri wa miaka 70 alianza kuugua akiwa ndani ya meli ya MV Hondius na kufariki alipowasili katika Kisiwa cha St Helena, huku mwili wake ukisubiri kurejeshwa nchini Uholanzi. Mke wake, mwenye umri wa miaka 69, pia aliugua na kufariki hospitalini mjini Johannesburg, Afrika Kusini. Wawili hao walikuwa raia wa Uholanzi.

    Kisa pekee kilichothibitishwa kuwa ni cha virusi hivyo ni ya raia wa Uingereza mwenye umri wa miaka 69 ambaye kwa sasa yuko hoi katika uangalizi maalum (ICU) jijini Johannesburg. Aidha, wahudumu wawili wa meli hiyo wanahitaji msaada wa haraka wa matibabu.

    Maafisa wa Uholanzi wanapanga kurejesha nchini mwao watu wawili wenye dalili pamoja na mwili wa mtu wa tatu aliyefariki ambao bado uko ndani ya meli hiyo.

    Virusi vya hantavirus huenezwa na panya, hasa kupitia hewa yenye chembechembe kutoka kinyesi au mkojo wa panya. Kwa kawaida, maambukizi kutoka mtu kwenda mtu ni nadra sana.

    Mtaalamu wa magonjwa ya kuambukiza, Profesa Paul Griffin, amesema hali hii ni ya kushangaza kwa sababu meli za kitalii zina mazingira yanayoweza kurahisisha maambukizi kutokana na msongamano wa watu, ingawa ni nadra sana kuona hantavirus ikisambaa katika mazingira kama hayo, hasa baada ya kuboreshwa kwa viwango vya usafi tangu janga la COVID-19.

  2. Iran yathibitisha kupokea jibu la Marekani kuhusu pendekezo lake jipya la amani

    Iran imetangaza kuwa imepokea majibu kutoka Marekani kufuatia pendekezo lake jipya la amani, huku msemaji wa wizara ya mambo ya nje akisema ujumbe huo uliwasilishwa kupitia Pakistan na sasa unafanyiwa tathmini.

    Hata hivyo, Marekani haijathibitisha rasmi kupokea au kujibu pendekezo hilo. Rais Donald Trump amenukuliwa akisema kuwa pendekezo au mpango huo wa iran haukubaliki kwake, akieleza kuwa haukidhi matarajio ya Washington.

    Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Iran, mpango huo wa vipengele 14 pamoja na mengine, unaitaka Marekani kuondoa majeshi karibu na mipaka ya Iran, kusitisha vikwazo kwenye bandari zake na kumaliza mashambulizi yote, ikiwemo yanayohusishwa na Israel nchini Lebanon.

    Pendekezo hilo pia linapendekeza makubaliano yafikiwe ndani ya siku 30, likihimiza pande zote kuzingatia kumaliza vita badala ya kuendeleza usitishaji mapigano wa sasa.

    Wakati huo huo, Trump amesema Marekani itaendelea kulinda usafirishaji wa meli katika Mlango wa Hormuz na kuonya kuwa kuna uwezekano wa kurejea kwa mashambulizi iwapo Iran “itafanya makosa”.

    Mvutano kati ya mataifa hayo unaendelea huku Iran ikikanusha madai ya kutengeneza silaha za nyuklia, wakati Marekani ikisisitiza kuwa haitaruhusu taifa hilo kuwa na silaha hizo.

  3. Marekani kusaidia meli zilizokwama Hormuz - Trump

    Rais wa Marekani Donald Trump ametangaza kuwa nchi yake itaanza operesheni maalum ya kusaidia meli zilizokwama katika Mlango bahari wa Hormuz, akieleza hatua hiyo ni kama “msaada wa kibinadamu” kwa mataifa yasiyohusika moja kwa moja na vita kati ya Marekani, Israel na Iran.

    Trump amesema operesheni hiyo itaanza rasmi leo Jumatatu, ikilenga kusaidia meli na wafanyakazi wake ambao wamekwama kwa zaidi ya miezi miwili kutokana na vizuizi vya Iran katika njia hiyo muhimu ya usafirishaji wa mafuta duniani.

    Katika ujumbe wake, Trump alisema Marekani itaziongoza meli hizo kupita salama ili ziweze kuendelea na shughuli zao, huku akionya kuwa jaribio lolote la kuingilia operesheni hiyo litakabiliwa na nguvu.

    Hatua hiyo inakuja wakati mvutano ukiendelea kuongezeka, ambapo Iran imezuia usafirishaji mafuta na bidhaa zingine kutoka Ghuba ya Uajemi, huku Marekani nayo ikiweka vikwazo kwa meli zinazotoka bandari za Iran.

    Wakati huo huo, Iran imethibitisha kuwa imepokea majibu kutoka Marekani kuhusu pendekezo lake la amani lenye masuala 14, likijumuisha madai ya kuondolewa kwa vikwazo na kusitishwa kwa mapigano, huku Tehran ikisema bado inalichambua jibu hilo.

    Hata hivyo, Trump ameashiria kutoridhishwa na pendekezo hilo la Iran, akisema huenda lisikubalike, wakati Iran ikisisitiza kuwa kwa sasa hakuna mazungumzo ya nyuklia hadi vita vitakapomalizika.

  4. Habari na karibu katika habari zetu za moja kwa moja leo Mei 04, 2026