Vozinha: Kipa "mzee" aliyeiteka dunia ya soka

    • Author, Elizabeth Conway
    • Nafasi, World Cup reporter
    • Akiripoti kutoka, Atlanta Stadium
  • Iliyochapishwa
  • Muda wa kusoma: Dakika 4

Kipyenga cha mwisho cha mchezo kilipopulizwa katika Uwanja wa Atlanta, kamera zote zilimlenga golikipa wa Cape Verde, Vozinha.

Machozi yalikuwa yakimtoka mwanasoka huyo mkongwe mwenye umri wa miaka 40 huku akianza kutambua ukubwa wa kile ambacho yeye na timu yake walikuwa wamekifanya baada ya kutoka sare ya bila kufungana dhidi ya Hispania, moja ya timu zinazopewa nafasi kubwa ya kutwaa Kombe la Dunia.

Mashabiki wa Cape Verde waliokuwa wamejaza sehemu kubwa ya uwanja walilipuka kwa furaha. Walikumbatiana, walicheza na kuimba huku wakisherehekea matokeo ambayo tayari yameingia katika historia ya taifa lao.

Uwanjani, wachezaji walikimbia huko na huko na kukumbatiana kwa furaha kubwa. Hata mashabiki wasiokuwa na upande wowote walijikuta wakivutiwa na simulizi ya Cape Verde na kuungana nao katika shangwe hizo.

Dhidi ya mabingwa wa Ulaya Hispania, golikipa mkongwe Vozinha alicheza kwa kiwango bora zaidi katika maisha yake ya soka, akiisaidia Cape Verde kupata sare ya kihistoria na kuweka rekodi ya matokeo makubwa zaidi kuwahi kufikiwa na taifa hilo la Afrika katika soka la kimataifa.

"Nililia kwa sababu nilikulia kwa babu na bibi yangu," alisema Vozinha baada ya kutangazwa mchezaji bora wa mechi.

"Kwa bahati mbaya hawapo tena duniani. Walifariki miaka michache iliyopita. Walikuwa kila kitu kwangu."

Aliongeza kuwa mama yake pia hakuweza kushuhudia tukio hilo muhimu.

"Mama yangu hakufanikiwa kufika hapa kutokana na masuala ya visa na gharama zake. Ningependa angekuwa hapa."

Vozinha alisema siri kubwa ya mafanikio ya Cape Verde ni umoja wao.

"Silaha yetu kubwa ni umoja. Haijalishi mchezaji amejiunga leo au amekuwa nasi kwa miaka mingi. Tunachukulia timu kama familia na hilo ndilo nguvu yetu kubwa."

"Watu wengi walidhani tumekuja Kombe la Dunia kwa ajili ya kujifurahisha tu. Lakini tumekuja kushindana na kupigania nchi yetu."

Ndoto ya utotoni iliyotimia

Kwa Vozinha, ambaye jina lake halisi ni Josimar Dias, huu ulikuwa wakati ambao ameusubiri maisha yake yote.

Golikipa huyo ameitumikia Cape Verde kwa miaka mingi akiwa na ndoto moja kubwa - kucheza Kombe la Dunia.

Ndoto hiyo ilmetimia, lakini imeambatana na historia nyingine. Akiwa na miaka 40 na siku 12, Vozinha alikua mchezaji mwenye umri mkubwa zaidi kucheza mechi ya kwanza ya Kombe la Dunia kwa taifa linaloshiriki kwa mara ya kwanza.

Ni golikipa wa Misri Essam El Hadary pekee aliyewahi kucheza mechi yake ya kwanza ya Kombe la Dunia akiwa na umri mkubwa zaidi.

Ni mafanikio makubwa kwa mwanasoka ambaye safari yake haikuwa rahisi.

"Nilianza kucheza soka la kulipwa nikiwa na miaka 25. Kwa mtu kama mimi huo ulikuwa umri wa kuchelewa sana," alisema.

"Nilifikiria kuachana na timu ya taifa mara kadhaa, lakini niliendelea kwa sababu ya ndoto hii."

Licha ya kutwaa tuzo ya mchezaji bora wa mechi, Vozinha alisema mafanikio hayo ni ya timu nzima.

"Mimi nimetajwa kuwa mchezaji bora, lakini tuzo hii ni ya wenzangu wote. Bila wao, hakuna chochote kingewezekana."

Ameipaisha Cape Verde

Cape Verde ni taifa la visiwa lililopo takribani kilomita 600 kutoka pwani ya magharibi mwa Afrika.

Likiwa na idadi ya watu inayozidi kidogo nusu milioni, ni moja ya mataifa madogo zaidi kuwahi kufuzu Kombe la Dunia.

Akiwa anakua katika mji wa Mindelo, Vozinha alikumbana na changamoto nyingi.

"Nilikuwa mmoja wa makipa bora kwenye kisiwa chetu, lakini nilikuwa mfupi," alikumbuka.

"Hata nilipocheza vizuri, sikupewa nafasi kwa sababu ya kimo changu."

Kama ilivyokuwa kwa wachezaji wengi wa Cape Verde, baadaye alihamia Ureno kutafuta nafasi zaidi za kucheza soka.

Safari hiyo ilimpeleka katika nchi mbalimbali ikiwemo Slovakia, Angola, Moldova na Cyprus kabla ya kujiunga na Chaves inayoshiriki ligi daraja la pili nchini Ureno.

Hata jina lake lina historia ya kipekee. Baba yake alitaka ampe jina la Valdano, kwa heshima ya nguli wa Argentina na Real Madrid Jorge Valdano.

Hata hivyo mamlaka za Cape Verde hazikukubali jina hilo na badala yake akaitwa Josimar, kwa heshima ya beki wa Brazil aliyeng'ara katika Kombe la Dunia la mwaka 1986.

Miongo kadhaa baadaye, Vozinha ameandika historia yake mwenyewe katika jukwaa hilo hilo la Kombe la Dunia.

"Ameifanya mechi kuwa ya kipekee"

Mbali na uwanjani, umaarufu wake uliongezeka kwa kasi katika mitandao ya kijamii.

Idadi ya wafuasi wake kwenye Instagram iliongezeka kutoka takribani 50,000 hadi zaidi ya milioni 1.5 baada ya kituo cha CazeTV nchini Brazil kuwahamasisha watazamaji wake kumfuatilia.

"Ni jambo la ajabu sana," alisema baada ya kupewa taarifa hiyo.

Mchezaji wa zamani wa Scotland Pat Nevin alisema Vozinha ndiye aliyeifanya mechi hiyo kuwa ya kipekee.

"Amekuwa wa kiwango cha juu kabisa. Kufanya haya akiwa na miaka 40 ni jambo la kushangaza," alisema.

Kwa taifa lenye wakazi zaidi kidogo ya nusu milioni, matokeo hayo yana umuhimu mkubwa sana.

Mashabiki waliovalia mavazi ya buluu na kubeba bendera za Cape Verde waliimba na kucheza kwa dakika zote 90, wakiisukuma timu yao katika kila wakati mgumu.

Na filimbi ya mwisho ilipopulizwa, haikuwa tena simulizi ya Cape Verde pekee.

Taifa dogo la visiwa, lenye ukubwa usiozidi mji wa Sheffield nchini Uingereza, lilikuwa limeiteka dunia ya soka.