Ruto afichua mradi mwingine wa Dangote baada ya kiwanda cha kusafisha mafuta cha Lamu

Chanzo cha picha, Ruto and X
Tajiri nambari moja barani Afrika, Aliko Dangote, yuko katika mazungumzo na serikali ya Kenya kwa ajili ya ujenzi wa bomba la mafuta ghafi litakalounganisha Lamu na Turkana, ikiwa ni sehemu ya mipango ya kufungua fursa za rasilimali ya mafuta nchini humo.
Rais William Ruto alibainisha hayo wakati wa mkutano na vyombo vya habari katika Ikulu Ndogo ya Kisumu siku ya Jumanne, Septemba 15, akisema bomba hilo linalopendekezwa litakuwa sehemu ya mradi wa kiwanda cha kusafisha mafuta ambacho Dangote anapanga kukijenga Lamu.
"Kama sehemu ya mradi huo wa kiwanda cha kusafisha mafuta huko Lamu, tunafanya mazungumzo na Dangote kuhusu ujenzi wa bomba la kuelekea Turkana ili tuweze kufaidika na mafuta tuliyonayo Turkana," alisema Ruto.
Rais pia alitangaza kuwa ujenzi wa kiwanda hicho utazinduliwa rasmi tarehe 30 Septemba, huku Dangote na viongozi wengine wa mataifa wakitarajiwa kuhudhuria hafla hiyo ya kuweka jiwe la msingi.










