Moja kwa moja, Hatuko vitani na Saudia na Wahouthi wana masuala yao wenyewe - Iran

Katika mahojiano na shirika la habari la India Today, Rais wa Iran Masoud Pezzekian amesema kuwa nchi yake haiko vitani na Saudia

Moja kwa moja

Abdalla Seif Dzungu

  1. Ruto afichua mradi mwingine wa Dangote baada ya kiwanda cha kusafisha mafuta cha Lamu

    .

    Chanzo cha picha, Ruto and X

    Maelezo ya picha, Mwekezaji Aliko Dangote na Rais William Ruto

    Tajiri nambari moja barani Afrika, Aliko Dangote, yuko katika mazungumzo na serikali ya Kenya kwa ajili ya ujenzi wa bomba la mafuta ghafi litakalounganisha Lamu na Turkana, ikiwa ni sehemu ya mipango ya kufungua fursa za rasilimali ya mafuta nchini humo.

    Rais William Ruto alibainisha hayo wakati wa mkutano na vyombo vya habari katika Ikulu Ndogo ya Kisumu siku ya Jumanne, Septemba 15, akisema bomba hilo linalopendekezwa litakuwa sehemu ya mradi wa kiwanda cha kusafisha mafuta ambacho Dangote anapanga kukijenga Lamu.

    "Kama sehemu ya mradi huo wa kiwanda cha kusafisha mafuta huko Lamu, tunafanya mazungumzo na Dangote kuhusu ujenzi wa bomba la kuelekea Turkana ili tuweze kufaidika na mafuta tuliyonayo Turkana," alisema Ruto.

    Rais pia alitangaza kuwa ujenzi wa kiwanda hicho utazinduliwa rasmi tarehe 30 Septemba, huku Dangote na viongozi wengine wa mataifa wakitarajiwa kuhudhuria hafla hiyo ya kuweka jiwe la msingi.

  2. China yaimarisha vikwazo vya usafiri kwa raia wake

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Sheria mpya zinazosimamia safari za kwenda na kutoka China zimeanza kutumika, hatua ambayo wachambuzi wanasema itaimarisha zaidi udhibiti wa serikali kwa raia wake.

    Raia wanaochukuliwa kuwa wame "dhuru" usalama wa taifa au maslahi ya China wakiwa nje ya nchi wanaweza pia kuzuiwa kuondoka China kwa muda wa hadi miaka mitatu baada ya kurejea, huku wale wanaokiuka kanuni za uingizaji na usafirishaji wa teknolojia wakikabiliwa na marufuku kama hiyo ya kutoweza kusafiri nje.

    Mamlaka za China zinasema sheria hizo zinalenga "kulinda mamlaka na usalama wa taifa" na zinakanusha madai kuwa zinazuia safari za "raia wa kawaida".

    Hata hivyo, wakosoaji wanasema sheria hizo mpya zinaweza kuongeza uwezo wa Beijing wa kushinikiza au kudhibiti shughuli za raia wake wakiwa nje ya nchi.

    "Hii ni nyenzo nyingine iliyoundwa kudhibiti kile ambacho raia wa China wanafanya na kusema wakiwa nje ya nchi," Profesa Tom Kellogg, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria za Asia katika Chuo Kikuu cha Georgetown, aliliambia shirika la BBC la lugha ya Kichina.

    "Katika baadhi ya matukio, ili kuwazuia watu binafsi kuikosoa serikali ya China wakiwa nje ya nchi au kuwaadhibu kwa shughuli zao za kutetea haki, mamlaka za usalama wa taifa hukataa moja kwa moja kutoa pasipoti," aliongeza Kellogg.

    Kwa mujibu wa sheria hizo zinazoanza kutumika siku ya Jumanne, raia wa China wanaweza kuzuiwa kuondoka nchini iwapo watakiuka kanuni za uingizaji na usafirishaji wa teknolojia ambazo "zinaweza kuhatarisha usalama wa viwanda au teknolojia wa taifa".

    Piyao, jukwaa la serikali ya China linaloshughulikia "ukanushaji wa uvumi", lilitoa taarifa wiki iliyopita likisema sheria hizo mpya "hazizuii safari za raia wa kawaida, bali zinatumika kama hatua ya tahadhari dhidi ya maeneo yenye hatari kubwa na watu binafsi wenye mwenendo usio wa kawaida wa kusafiri".

  3. Israel yatangaza kuuawa kwa kamanda wa kijeshi wa Hamas huko Gaza

    .

    Chanzo cha picha, Ayman Majed Harb Alhisi/Anadolu via Getty Images

    Maelezo ya picha, Jumanne asubuhi, ndege isiyo na rubani ya Israeli ililenga gari hilo katika kitongoji cha al-Saftawi kaskazini mwa Jiji la Gaza.

    Jeshi la Israel lilitangaza siku ya Jumatatu kuwa limewaua wanachama watano wa Hamas, akiwemo kamanda wa kijeshi, katika operesheni huko Gaza.

    Gazeti la *The Times of Israel* liliripoti kuwa jeshi la Israel lilitangaza kuwa vikosi vyake na shirika la usalama wa ndani la Israel, Shin Bet, vimeongeza kasi ya "operesheni zao za kupambana na ugaidi" katika Ukanda wa Gaza katika wiki za hivi karibuni.

    Kamanda wa kijeshi wa Hamas ambaye gari lake liliripotiwa kulengwa na Israel ni "Ahmad al-Batsh," anayejulikana kwa jina la utani "Abu Osama," na vyanzo vya habari vya Hamas pia vimethibitisha kifo chake.

    Shirika la Habari la Fars - ambalo lina uhusiano wa karibu na Walinzi wa Mapinduzi - liliandika usiku wa Jumatatu, likinukuu "Gaza Al-Aan", kwamba alikuwa kamanda wa Vikosi vya Izz al-Din al-Qassam na aliuawa kufuatia shambulio la anga la Israel.

    Al Jazeera pia iliandika kuhusu namna ambavyo mwanachama huyo mwandamizi wa Hamas aliuawa, ikisema kuwa aliuawa katika "shambulio la anga dhidi ya gari katika Mtaa wa Al-Saftawi, ulioko kaskazini mwa Jiji la Gaza (magharibi mwa Jabalia)."

  4. Trump asema hofu kuhusu usalama wa akili mnemba ni 'uzushi'

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Rais Donald Trump

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema kuwa hofu kuhusu usalama wa Akili Bandia (AI) ni "uzushi", huku akikosoa wito wa kuwepo kwa hatua zaidi za udhibiti kwa teknolojia hiyo inayokua kwa kasi.

    Kauli hiyo imekuja baada ya Jack Clark, mwanzilishi mwenza wa kampuni kubwa ya AI iitwayo Anthropic, kuiambia BBC kuwa huenda ikahitajika kuweka sheria ya lazima katika sekta hiyo ya kuwa na "kitufe cha kuzima" (kill switch) kwa mifumo hatari ya AI, ambacho kinaweza kukaguliwa na upande wa tatu.

    Maoni ya Clark yalifuatia maonyo kuhusu hatari ambazo teknolojia hiyo inaleta kwa binadamu, maonyo yaliyotolewa hivi karibuni na watendaji pamoja na wafanyakazi kadhaa katika kampuni zinazoongoza kwenye sekta ya AI.

    Hofu hizo zilisababisha mauzo makubwa ya hisa za baadhi ya kampuni za teknolojia siku ya Jumatatu, huku wawekezaji wakitathmini athari zinazoweza kutokea kutokana na uwezekano wa kupungua kwa kasi ya maendeleo ya AI.

    Katika mfululizo wa machapisho kwenye mitandao ya kijamii siku ya Jumatatu, Rais wa Marekani alilinganisha maonyo kuhusu AI na "Uzushi wa Kupanda kwa Joto Duniani" (Global Warming Scam), jambo ambalo alisema "linaendelezwa na Wademokrat wenye msimamo mkali wa kushoto na wapumbavu" (Radical Left Dumocrats).

    Trump pia alijiita "Mvumbua Uzushi" (Hoax Buster), akilinganisha hofu kuhusu usalama wa teknolojia hiyo na kile alichokiita "Uzushi wa URUSI, URUSI, URUSI".

    Katika chapisho jingine aliandika: "Kuna njama CHAFU zinazoendelea dhidi ya AI na Vituo vya Data, na pekee anayefurahia hilo ni China. YEYOTE ATAKAYESHINDA KWENYE AI, NDIYE ATAKAYESHINDA!"

    Na mapema siku ya Jumatatu, Trump aliandika kwenye mitandao ya kijamii kuwa "hatua pekee za udhibiti" zinazohitajika kwa ajili ya AI ni kuwa na rais "imara na mwenye akili".

  5. IRGC yasema meli kubwa ya mafuta iligonga bomu la majini na kulipuka kusini mwa Hormuz

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, IRGC

    IRGC yasema meli kubwa ya mafuta iligonga bomu la majini na kuwaka moto kusini mwa Mlango-bahari wa Hormuz

    Kamandi ya Jeshi la Wanamaji la IRGC ameeleza katika taarifa kwamba meli kubwa ya mafuta iitwayo "Algaya" iligonga migodi ya majini katika njia ya kusini ya Mlango-bahari wa Hormuz na kupata ajali.

    Kwa mujibu wa taarifa kutoka Jeshi la Wanamaji la IRGC, "Jaribio la kudhibiti moto huo halikufanikiwa na meli hiyo yote iliteketea kwa moto."

    Iran inasema kuwa kupita katika njia hiyo ya kusini—ambayo Oman imetangaza kuwa yake na ambayo Marekani inadai kuilinda ni jambo "hatari" na "haramu."

    Katika taarifa yake, IRGC ilisisitiza kuwa Mlango-bahari wa Hormuz bado "umefungwa."

    Wakati huo huo, CENTCOM ambayo ni Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani imekanusha ripoti ya Walinzi wa Mapinduzi (IRGC) kuhusu suala hilo na kuelezea madai ya kushambuliwa kwa meli hiyo katika Mlango-bahari wa Hormuz kama "uongo."

  6. Tetesi: Atletico Madrid na Juventus zamtaka Noni Madueke

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Mchezaji wa Arsenal Noni Madueke

    Atletico Madrid na Juventus wanatafakari uwezekano wa kumsajili kwa mkopo mwezi Januari mshambuliaji wa Arsenal na England, Noni Madueke, mwenye umri wa miaka 24. (Caught Offside)

    Liverpool, Bayern Munich na Real Madrid zote zina nia ya kuimarisha safu yao ya kiungo kwa kumsajili mchezaji wa kimataifa wa Austria mwenye umri wa miaka 20, Paul Wanner, anayechezea PSV Eindhoven. (Teamtalk, External)

    Lazio wameanza tena mazungumzo na mshambuliaji wa Argentina, Mauro Icardi, ambaye ni mchezaji huru baada ya kuondoka Galatasaray, na mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 33 yuko tayari kwa uhamisho huo. (Sky Sports Italia, External)

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Mauro Icardi

    Everton pia wamehusishwa na Icardi lakini kocha wa timu hiyo, David Moyes, anasita kuingia sokoni kutafuta wachezaji huru kwa sasa. (Football Insider External)

    Crystal Palace wanalenga kumpatia kipa wa England, Dean Henderson, mwenye umri wa miaka 29, mkataba mpya. (The Athletic – Subscription Required External)

    Nottingham Forest watamsajili mshambuliaji wa Shamrock Rovers, Michael Noonan, mwenye umri wa miaka 18, kwa utaratibu wa fidia ya mafunzo mwezi Januari. (Irish Mirror, External)

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, David Moyes

    Inter Milan wako katika mazungumzo ya kuongeza mikataba ya mchezaji wa upande wa kushoto wa Italia, Federico Dimarco (28), na kiungo wa Uturuki, Hakan Calhanoglu (32). (Football Italia, External)

    Aliyekuwa mshambuliaji wa Ufaransa, Karim Benzema (38), amezungumza na wachezaji wa Bayer Leverkusen huku akitafuta klabu mpya baada ya kuondoka Al-Hilal katika kipindi cha majira ya joto. (Fichajes – In Spanish, External)

  7. Hatuko vitani na Saudia na Wahouthi wana masuala yao wenyewe - Iran

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Rais Pezzekssian

    Katika mahojiano na shirika la habari la India Today, Rais wa Iran Masoud Pezzekian amesema kuwa nchi yake haiko vitani na Saudai , na kwamba nchi za eneo hilo pia zina "mtazamo potofu" kuhusu mashambulizi ya Iran dhidi ya kambi za kijeshi za Marekani katika eneo hilo.

    Katika mazungumzo hayo, ambayo yalirekodiwa wakati Bw. Pezzekian akiwa nchini India kuhudhuria mkutano wa kilele wa BRICS na kurushwa hewani na mashirika ya habari ya Iran siku ya Jumatatu, Bw. Pezzekian anasema: "Hatuko vitani na Saudi Arabia, na Wahouthi pia wana masuala yao wenyewe. Nchi zote za eneo hilo zinapaswa kukaa pamoja na kuleta amani na usalama katika eneo hilo. Hakuna mantiki wala sababu ya sisi kuwa katika vita na migogoro sisi kwa sisi."

    Rais wa Iran amesisitiza: "Tatizo ni kwamba Marekani imeanzisha kambi katika ardhi ya nchi za Kiarabu. Wanatushambulia kutokea huko. Haiwezekani tukawa tunashambuliwa kutokea huko kila siku. Sisi hatukuwashambulia wao. Tulilenga chanzo cha shambulio dhidi ya nchi yetu. Kwa kawaida, jambo hili limesababisha kiasi fulani cha chuki dhidi ya nchi za eneo hilo."

  8. Ndege za kivita za NATO zaangusha ndege isiyo na rubani iliyoingia katika anga ya Lithuania

    .

    Chanzo cha picha, AFP Via Getty

    Marubani wa ndege za kivita za NATO wameidungua ndege isiyo na rubani (drone) iliyoingia katika anga ya Lithuania usiku kucha, Rais wa Lithuania amesema.

    Mamlaka zimesema kuwa ndege hiyo huenda iliingia kusini mwa Lithuania, karibu na jiji la pili kwa ukubwa la Kaunas, ikitokea nchi jirani ya Belarus muda mfupi baada ya saa sita usiku siku ya Jumanne.

    Rais wa Lithuania, Gitanas Nausėda, aliandika katika taarifa kwenye mtandao wa X: "Ndege isiyo na rubani iliyoingia katika anga ya Lithuania imeangamizwa na ndege za kivita za NATO."

    Chanzo cha ndege hiyo bado hakijajulikana, msemaji wa kituo cha kitaifa cha usimamizi wa dharura cha Lithuania alisema.

    Tahadhari kuhusu ndege hiyo zilisikika katika mji mkuu wa Vilnius na maeneo ya jirani mapema siku ya Jumanne.

    Jeshi la Lithuania na marubani wa Italia wanaohudumu katika Operesheni ya NATO ya Ulinzi wa Anga "walionyesha mwitikio wa haraka na wa uwajibikaji" dhidi ya kuingia kwa ndege hiyo, Wizara ya Ulinzi ya Lithuania ilisema.

    Ujumbe wa Nausėda kwenye mitandao ya kijamii uliongeza: "Wakati Urusi ikiongeza uchokozi wake dhidi ya Ukraine, utayari wa namna hii ni muhimu sana kwa eneo letu. Kwa kushirikiana na washirika wetu wa NATO, Lithuania italinda anga yake."

    Moscow haijatoa maoni yoyote kuhusu tukio hilo.

  9. Marekani yathibitisha kupeleka silaha anga za juu

    ..

    Chanzo cha picha, Thomas Traasdahl/Ritzau Scanpix/AFP via Getty Images

    Marekani imethibitisha kuwa imetuma silaha ya angani katika obiti ya Dunia, ikiwa ni mara ya kwanza kukiri kuwa na uwezo kama huo wa mashambulizi.

    Waziri wa Jeshi la Anga la Marekani, Troy Meink, amesema silaha hiyo iliyopo kwenye obiti ilikuwa muhimu ili kulinda vikosi vya Marekani dhidi ya vitendo vya uhasama vya adui.

    Akizungumza katika Kongamano la Anga, Nafasi ya Anga na Mtandao (Air, Space and Cyber ​​Conference) siku ya Jumatatu, Meink alisema Marekani iko tayari kukabiliana na "vitisho vinavyobadilika", lakini hakutoa maelezo zaidi kuhusu uwezo wa silaha hiyo au wakati ilipowekwa kwenye obiti.

    Viongozi wa ngazi ya juu wa kijeshi hapo awali walisema walipanga kuimarisha uwezo wa kijeshi angani, wakitaja mipango ya Urusi na China ya kutengeneza njia za kushambulia na kuvuruga satelaiti za Marekani katika mzozo wa siku zijazo.

    Utawala wa Trump umesema kuwa uwezo wa kijeshi wa angani - na makombora ya kuzuia mashambulizi - ni sehemu muhimu ya mfumo wake wa ulinzi unaopangwa kuitwa "Golden Dome" ili kuilinda Marekani dhidi ya makombora na vitisho vingine vya angani.

    Mkataba wa mwaka 1967 ulipiga marufuku silaha za maangamizi makubwa katika obiti. Tangu wakati huo, mataifa yenye nguvu kubwa ikiwemo Marekani, Urusi, na China yamekuwa yakichunguza uwezo mwingine nje ya mkataba huo, kama vile kulenga satelaiti za wapinzani - ambazo ni muhimu kwa mawasiliano ya kijeshi, ufuatiliaji na urambazaji.

    Mwaka jana, Rais Donald Trump alitoa agizo la kiutendaji likisisitiza jukumu la Jeshi la Anga la Marekani (US Space Force) si tu katika kulinda rasilimali, bali pia kama nguvu ya kushambulia.

    Jeshi la Anga la Marekani - tawi jipya zaidi la jeshi la Marekani katika kipindi cha zaidi ya miaka 70 - lilianzishwa mwaka 2019 kama njia ya kulinda rasilimali za Marekani angani, ikiwa ni pamoja na mamia ya satelaiti zinazotumiwa kwa mawasiliano na ufuatiliaji.

  10. Natumai hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja