Mahakama nchini Canada kusikiliza kesi ya Thomas Partey kunyimwa viza
Mahakama nchini Canada inatarajiwa kusikiliza kesi iliyowasilishwa na serikali ya Ghana ikiomba kutathminiwa upya kwa hatua ya mchezaji wake Thomas Partey kunyimwa viza. S
erikali inaomba Partey kuruhusiwa kuingia Canada kwa muda mfupi ili kushiriki katika mchezo wa ufunguzi wa timu ya taifa ya Ghana dhidi ya Panama siku ya Jumatano.
Pia wanaomba mahakama kuiagiza mamlaka ya uhamiaji ya Canada kumruhusu Partey kuwasilisha ombi jipya la viza.
Kunyimwa viza kwa Partey kunahusishwa na kesi za uhalifu dhidi yake nchini Uingereza, ambapo anakabiliwa na mashtaka ya ubakaji na unyanyasaji wa kijinsia.
Mchezaji huyo wa zamani wa Arsenal, ambaye sasa anachezea Villarreal ya Uhispania, amekanusha mashitaka yote na anatarajiwa kusomewa mashitaka mwaka ujao nchini Uingereza.
Serikali ya Ghana katika taarifa yake siku ya Jumamosi ilielezea uamuzi wa Canada wa kumnyima Thomas Partey viza kuwa ‘‘uonevu na usio wa haki’’, ikisema ulitokana na madai ambayo hayajajaribiwa mahakamani.
Katika taarifa kwa BBC, Mamlaka ya Uhamiaji, Wakimbizi na Uraia wa Canada ilisema: ‘’Canada inazingatia sheria zake kikamilifa, kuandaa Kombe la Dunia hakujabadilishi sheria zake uhamiaji. Kila mtu anayetaka kuzuru Canada anafanyiwa tathmini ya kibinafsi, kwa mujibu wa sheria.’
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ghana, Samuel Okudzeto Ablakwa, amesema kuwa nchi hiyo pia inatumia njia za kidiplomasia kumtafutia Thomas Partey viza ya Canada.
Partey amekuwa mchezaji muhimu katika timu ya taifa ya soka ya Ghana, Black Stars na kukosekana kwake uwanjani kutakuwa na thari.
Wachambuzi wanaamini kwamba anaweza kukosa michezo mingi ikiwa Ghana itafuzu zaidi ya hatua ya makundi katika michuano hiyo.
Soma zaidi: