Milipuko na milio ya risasi imeripotiwa katika mji mkuu wa Mali, Bamako, huku makundi yenye silaha yakianzisha mashambulizi yanayoonekana kuratibiwa katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Katika taarifa yake siku ya Jumamosi, jeshi la nchi hiyo lilisema “mapigano yanaendelea,” likiongeza kuwa “vikosi vyetu vya ulinzi na usalama kwa sasa vinapambana kuwazuia washambuliaji.”
Kwa mujibu wa Reuters, mashuhuda wanasema kuwa milipuko na risasi zilisikika karibu na kambi ya kijeshi, kambi kubwa iliyopo nje kidogo ya mji mkuu. Wanajeshi wamepelekwa kufunga barabara katika eneo hilo.
Pia kuna taarifa za mashambulizi katika mji wa Gao mashariki, Kidal kaskazini na Sevare katikati mwa Mali, katika kile ambacho mchambuzi mmoja amekielezea kuwa ni shambulio kubwa zaidi la wanamgambo wa jihadi kwa miaka ya hivi karibuni.
Mkazi mmoja aliyekuwa akisafiri kurejea Bamako kutoka Ethiopia aliiambia BBC kuwa safari zote za ndege kuelekea mji huo zilifutwa mapema Jumamosi. Bado haijabainika wazi kama mashambulizi hayo yameathiri uwanja wa ndege.
Ubalozi wa Marekani nchini Mali umewashauri raia wake kubaki walipo na kuepuka safari, ukitaja milipuko na milio ya risasi karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Modibo Keita mjini Bamako na maeneo ya kati ya nchi.
Ulf Laessing, mkuu wa Mpango wa Sahel katika Konrad Adenauer Foundation nchini Mali, ameiambia BBC kuwa tukio hilo linaonekana kuwa “shambulio kubwa zaidi lililoratibiwa na wanamgambo wa jihadi nchini Mali kwa miaka kadhaa.”
Jeshi la Mali limesema linapambana na “makundi ya kigaidi” ambayo hayajatambuliwa, ingawa maelezo zaidi bado hayajawekwa wazi. Video zinazosambaa mitandaoni zinaashiria uwepo wa kundi la jihadi la Jama'at Nusrat al-Islam wal-Muslimin (JNIM) pamoja na waasi wa Tuareg wa Azawad Liberation Front (FLA).