'Hii ndiyo sababu yeye ni mfalme' – Messi alivyoiwezesha Argentina kufuzu fainali ya tatu ya Kombe la Dunia

Messi

Chanzo cha picha, Getty Images

Iliyochapishwa
Muda wa kusoma: Dakika 6

Miaka minne iliyopita, ilionekana kana kwamba simulizi ya Lionel Messi ilikuwa imefikia mwisho.

Hatimaye alikuwa ameshinda Kombe la Dunia akiwa na umri wa miaka 35, katika kile alichosema kuwa ulikuwa mchezo wake wa mwisho kwenye mashindano hayo.

Kwa mtazamo wa wengi, ushindi huo uliimarisha nafasi yake kama mchezaji bora zaidi kuwahi kutokea katika historia ya soka.

Miaka minne kabla ya hapo, akiwa na umri wa miaka 31, wengi, wakiwemo watu wa karibu naye, waliamini kuwa tayari alikuwa amecheza mchezo wake wa mwisho wa Kombe la Dunia na angehitimisha maisha yake ya soka bila kutwaa taji hilo.

Lakini sasa, akiwa na umri wa miaka 39, Messi ameisaidia Argentina kuifunga England na kufuzu fainali ya pili mfululizo ya Kombe la Dunia.

Pasi zake mbili zilizozaa mabao ziliisaidia Argentina kutoka nyuma na kushinda kwa mabao 2-1, na hivyo kumfikisha Messi kwenye pasi nne za mabao katika Kombe la Dunia la 2026, sambamba na mabao yake manane.

Hilo linamfanya kuwa mfungaji wa pamoja anayeongoza katika mashindano hayo, huku pia akiwa mchezaji wa pili kwa kutoa pasi nyingi za mabao.

Argentina itacheza na Hispania, nchi ambayo Messi ametumia sehemu kubwa ya maisha yake ya soka akiwa na Barcelona, katika fainali itakayochezwa Jumapili mjini New Jersey.

Kocha wa Argentina, Lionel Scaloni, alisema:

"Yeye ndiye mchezaji bora zaidi katika historia. Sijui ni nini kingine anachopaswa kufanya ili kuthibitisha hilo. Wahispania wengi wanampenda."

Mchambuzi wa BBC, Micah Richards, alisema:

"Wana Lionel Messi. Wana 'GOAT', yaani mchezaji bora zaidi wa wakati wote."

Aliongeza:

"Soka huamuliwa na nyakati muhimu. Tulidhani huenda zingekuwa za Jude Bellingham au Harry Kane, lakini hii ndiyo sababu Messi ndiye mfalme."

Hauhitaji Whatsapp
BBC Swahili sasa kwenye WhatsApp

Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.

Bonyeza hapa kujiunga

Mwisho wa Whatsapp

Messi, ambaye aliwahi kuichezea Barcelona na Paris Saint-Germain, hakuwa amewahi kucheza dhidi ya England katika maisha yake ya soka kabla ya mechi hii.

Baada ya mchezo huo, kocha Thomas Tuchel na mashabiki wa England huenda walitamani hali hiyo ingebaki hivyo.

Mkongwe huyo alionesha ubora wake mara kadhaa katika kipindi cha kwanza, akicheza zaidi katikati ya uwanja. Hata hivyo, baada ya Anthony Gordon kuipa England bao la kuongoza katika dakika ya 55, Argentina ilianza kutawala mchezo.

Tuchel alipowaleta mabeki zaidi na England kuamua kujilinda, Argentina ilimiliki mpira kwa asilimia 88 katika dakika 37 zilizofuata.

Messi aling'ara zaidi baada ya kuhamia upande wa kulia wa uwanja.

Mlinda lango wa Argentina, Emiliano Martínez, alisema baada ya mechi:

"Kumhamishia Messi upande wa winga kulikuwa chanzo cha ushindi wetu."

Dhidi ya England, Messi alikamilisha chenga tisa zilizofanikiwa na kutoa pasi mbili za mabao.

Hivyo akawa mchezaji wa kwanza, kwa mujibu wa takwimu zilizorekodiwa tangu mwaka 1966, kufanya hivyo katika mchezo mmoja wa hatua ya mtoano wa Kombe la Dunia.

Kwa kulinganisha, timu nzima ya England ilikamilisha chenga saba tu zilizofanikiwa katika mechi hiyo iliyochezwa Atlanta.

Messi pia aligusa mpira mara saba ndani ya eneo la hatari la wapinzani, idadi sawa na miguso yote ya wachezaji wa England kwa pamoja. Vivyo hivyo, alitengeneza nafasi nne za mabao, sawa na timu nzima ya England.

Aidha, alipiga krosi tisa, nyingi zaidi kuliko mchezaji mwingine yeyote uwanjani.

Muhimu zaidi, alihusika moja kwa moja katika mabao yote mawili ya Argentina.

Bao la kwanza lilitokana na mpira wa kona, ambapo alimpa pasi Enzo Fernández, aliyefunga bao la kusawazisha katika dakika ya 85 kwa mkwaju kutoka nje ya eneo la penalti.

Kisha, katika dakika za nyongeza, Messi alipiga krosi iliyomkuta Lautaro Martínez, ambaye aliifungia Argentina bao la ushindi kwa kichwa.

Mchezaji wa zamani wa England, Micah Richards, alisema:

"Anatembea tu uwanjani, lakini mpira unapofika miguuni mwake anabadilika kabisa. Kipaji chake cha kipekee hujitokeza, na mara nyingi hicho ndicho kinachoamua matokeo ya mchezo."

Kipa wa zamani wa England, Joe Hart, aliongeza:

"England walirudi kwenye mfumo walioutumia dhidi ya Mexico na Norway, wakijilinda sana. Lakini kufanya hivyo kulimpa Lionel Messi uhuru. Yeye ndiye aliyekuwa na ufunguo wa kufungua ulinzi, na alitawala kabisa mchezo katika dakika 15 za mwisho."

Nahodha wa England, Harry Kane, alisema:

"Kwa sehemu kubwa ya mchezo tulimdhibiti vizuri. Lakini kama ilivyo kwa wachezaji hatari zaidi duniani, anapokuwa na mpira anaweza kutengeneza jambo maalumu. Kuna sababu inayomfanya awe mmoja wa wachezaji bora zaidi kuwahi kutokea."

Je, Messi anaweza kushinda Kiatu cha Dhahabu?

Lionel Messi ndiye mfungaji bora wa muda wote wa timu ya taifa ya Argentina, akiwa amefunga mabao 125

Chanzo cha picha, Getty Images

Majira haya ya kiangazi, Messi alikua mfungaji bora wa muda wote katika historia ya Kombe la Dunia, akiwa amefikisha mabao 21, kati ya jumla ya mabao 125 aliyofunga akiwa na timu ya taifa ya Argentina.

Kati ya mabao hayo 21, 15 ameyafunga tangu alipotimiza miaka 35.

Katika Kombe la Dunia la mwaka huu pekee, amefunga mabao manane, akivuka rekodi yake ya mabao saba aliyofunga mwaka 2022, ambapo alikosa Kiatu cha Dhahabu kwa bao moja nyuma ya Kylian Mbappé.

Safari hii, Messi na Mbappé wana mabao manane kila mmoja. Ufaransa ya Mbappé itacheza dhidi ya England siku ya Jumamosi katika mechi ya kuwania nafasi ya tatu.

Wachezaji wa England, Jude Bellingham na Harry Kane, kila mmoja ana mabao sita, hivyo bado wana nafasi ya kuwania Kiatu cha Dhahabu.

Iwapo wachezaji watamaliza mashindano wakiwa na idadi sawa ya mabao, mshindi ataamuliwa kwa kuangalia idadi ya pasi za mabao. Kwa sasa, Messi ana pasi nne za mabao, huku Mbappé akiwa na tatu.

Messi pia anaweza kumaliza mashindano akiwa kinara wa kutoa pasi za mabao, ingawa kwa sasa yuko nyuma kwa pasi moja dhidi ya Michael Olise wa Ufaransa.

Akizungumza na BBC, mlinda lango wa zamani wa England, Paul Robinson, alisema:

"Yeye ni mchawi mdogo, kweli kabisa. Ameonesha hilo katika mashindano yote. Ukiangalia mabao aliyofunga na mipira aliyoipeleka kwenye eneo la hatari la England, utaona ubora wake."

Je, Messi atapunguza kasi siku moja?

Ni rahisi kusahau kwamba mwaka 2016, Lionel Messi, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 29 na akiichezea Barcelona, alitangaza kustaafu soka la kimataifa.

Kabla ya uamuzi huo, alikuwa amepoteza fainali ya Kombe la Dunia ya mwaka 2014 dhidi ya Ujerumani pamoja na fainali tatu za Copa América.

Baada ya kubadili uamuzi wake na kurejea katika timu ya taifa, aliiongoza Argentina kutwaa mataji mawili ya Copa América.

Messi, ambaye wakati huo alikuwa mchezaji wa Paris Saint-Germain (PSG), alipoinua Kombe la Dunia nchini Qatar mwaka 2022, wengi walihisi kuwa alikuwa amekamilisha kipande cha mwisho cha mafanikio katika maisha yake ya soka.

Kwa wengi, ushindi huo uliondoa hoja ya mwisho iliyokuwa ikijadiliwa kuhusu nani ndiye mchezaji bora zaidi kuwahi kutokea, huku baadhi ya watu wakiendelea kuwaona Pelé na Diego Maradona kuwa wakubwa zaidi kutokana na mafanikio yao ya Kombe la Dunia.

Kabla ya fainali ya mwaka 2022, Messi alisema:

"Nina furaha sana kumaliza safari yangu ya Kombe la Dunia katika fainali. Kucheza mchezo wangu wa mwisho wa Kombe la Dunia ukiwa fainali ni jambo linalonipa furaha kubwa."

Aliongeza:

"Kuna miaka mingi kati ya sasa na Kombe la Dunia lijalo. Sidhani kama nitaweza kufika huko. Kumaliza safari yangu kwa namna hii ni jambo la ajabu."

Alipoondoka Ulaya mwaka uliofuata na kujiunga na Inter Miami inayoshiriki Ligi Kuu ya Marekani (MLS), wengi walidhani kuwa alikuwa ameanza kuelekea mwisho wa maisha yake ya soka.

Hata wakati wa Kombe la Dunia la Klabu la FIFA mwaka jana, aliloshiriki, haikuwa wazi kama angekuwepo katika Kombe la Dunia la mwaka huu.

Lakini sasa yuko hapa tena, akiendelea kung'ara kana kwamba hawezi kuzuilika, licha ya mtindo wake wa uchezaji kubadilika.

Kabla ya mechi dhidi ya England, takwimu zilionesha kuwa Messi alitembea kwa asilimia 47 ya umbali wote alioufanya katika mashindano haya, asilimia kubwa zaidi kuliko mchezaji mwingine yeyote wa uwanjani.

Mwandishi wa habari wa Hispania, Guillem Balagué, ambaye ameandika wasifu wa Messi, anasema kuwa Messi amejibadilisha kimtindo angalau mara tano katika maisha yake ya soka.

Kwa sasa, Messi amefunga bao au kutoa pasi ya bao katika mechi 13 mfululizo akiwa na Inter Miami na timu ya taifa ya Argentina.

Iwapo atahusika katika bao lolote kwenye fainali dhidi ya Hispania Jumapili, atasawazisha rekodi yake mwenyewe ya mwaka 2011 ya kushiriki katika mabao katika mechi 14 mfululizo.

Pia atakuwa mchezaji wa pili baada ya Cafu kucheza fainali tatu za Kombe la Dunia.

Je, hiyo ndiyo itakuwa mechi yake ya mwisho ya Kombe la Dunia? Baada ya yote, atakuwa na umri wa miaka 43 mwaka 2030.

Lakini pengine, kwa hatua aliyofikia mshindi huyo wa mara nane wa tuzo ya Ballon d'Or, ni bora kuacha kudhani chochote kuhusu kile anachoweza au hawezi kufanya.