Waziri mkuu wa Lebanon ameishutumu Israeli kwa uhalifu wa kivita baada
ya mashambulizi ya anga ya Israeli kumuua mwandishi mmoja wa habari na
kumjeruhi mwingine kusini mwa Lebanon siku ya Jumatano.
Maafisa nchini Lebanon wanasema Amal Khalil na Zeinab Faraj walishambuliwa
kimakusudi walipokuwa wakitafuta hifadhi katika nyumba baada ya shambulio la
awali la anga kupiga gari lililokuwa mbele yao, na kuwaua wanaume wawili.
Maafisa hao pia wanalishutumu Jeshi la Ulinzi la Israeli (IDF) kwa kushambulia
ambulensi kwa makusudi ilipojaribu kuwafikia waandishi wa habari katika kijiji
cha Tayri.
Jeshi la IDF limekana kwamba limezuia timu za uokoaji kufika katika eneo
hilo na kusema haliwalengi waandishi wa habari.
Waandishi wa habari Khalil, 43, ambaye alifanya kazi katika gazeti la
Lebanoni la Al-Akhbar, na Faraj, mpiga picha huru, walikuwa wakisafiri pamoja.
Wanaume wawili waliofariki hawajatajwa majina.
Mapema mwezi huu, waandishi wa habari wawili waliuawa katika
mashambulizi tofauti ya Israel nchini Lebanon.
Mwezi uliopita, waandishi wa habari watatu wa Lebanon waliuawa
katika shambulio la Israel katika mji wa Jezzine, waajiri wao walisema.
Kwa uchache watu 2,475 wameuawa katika mashambulizi ya Israeli nchini
Lebanon tangu vita vya hivi karibuni vianze, na zaidi ya 7,500 wamejeruhiwa,
kulingana na mamlaka ya Lebanon. Idadi hiyo inajumuisha wanawake 274 na watoto 177.