Bomu la Marekani huenda lilipiga harusi nchini Iran kimakosa - Gazeti la Washington

Chanzo cha picha, Iranian Red Crescent Society
Gazeti la Washington Post limeripoti kwa njia ya kipekee siku ya Jumapili kuwa uchunguzi wa awali unaonyesha shambulio lililosababisha vifo katika harusi katika mji wa Kohstak, kusini mwa Iran, huenda lilitokea baada ya moja ya mabomu sita yaliyoongozwa kwa usahihi, yaliyorushwa na ndege za kivita za Jeshi la Wanamaji la Marekani, kupotoka na kukosa shabaha iliyokusudiwa.
Kwa mujibu wa gazeti hilo, silaha sita za Marekani zililenga jengo la mawasiliano na huduma za simu lililokuwa karibu na eneo la sherehe, lakini moja ya mabomu hayo ilikosa shabaha na kulipiga jengo ambako sherehe ya harusi ilikuwa ikiendelea.
Washington Post, likimnukuu mtu anayefahamu kwa karibu maelezo ya operesheni hiyo, liliripoti kuwa tathmini ya awali ya jeshi la Marekani ilionyesha kuwa tukio hilo lilisababishwa na "kosa la kombora" na si "kulengwa kwa makusudi kwa jengo ambako sherehe ilikuwa ikiendelea."
Ripoti hiyo imechapishwa wakati Kamandi Kuu ya Marekani, CENTCOM, ikisema inachunguza taarifa kuhusu vifo vya raia vilivyosababishwa na shambulio hilo. Maafisa wa Marekani wamesema matokeo ya mwisho ya uchunguzi huo bado hayajatolewa.





















