Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Iran yaonya dhidi ya meli za Marekani zinazokaribia mlango wa Hormuz

Ali Mohammadi, naibu afisa wa masuala ya kisiasa katika Jeshi la Wanamaji la Walinzi wa Mapinduzi (IRGC), akirejelea kauli za Rais wa Marekani Donald Trump kuhusu kudhibiti wa Lango la Hormuz, alisema: "Ikiwa ndivyo ilivyo, kwa jina la Mungu, leteni mojawapo ya meli zenu ndani ya umbali wa kilomita 100."

Muhtasari

  • Senegal ipo tayari kwa michezo ya Olimpiki ya vijana 2026
  • 6 wafariki, 107 waokolewa kwenya ajali katika kivuko kwenye Bahari ya Java, Indonesia
  • Akili unde yatishia maisha ya binadamu, wasema wataalamu
  • Uganda yaamrisha wanafunzi kutoka DRC kuwekwa karantini kwa siku 21 kabla ya kurejea shuleni
  • Homa ya nguruwe yawaua nguruwe 1500 Kenya
  • Tetesi: Arsenal kushindana na Real Madrid katika kumsajili Nico Paz
  • Vuguvuu la kisiasa nchini Kenya Linda mwanachi lazuru Nairobi
  • Wahouthi watangaza mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani dhidi ya kambi ya kijeshi ya Saudia
  • Iran yaonya dhidi ya meli za Marekani zinazokaribia mlango wa Hormuz

Moja kwa moja

Abdalla Seif Dzungu

  1. 6 wafariki, 107 waokolewa kwenya ajali ya kivuko huko Java, Indonesia

    Watu sita wamefariki dunia huku wengine 107 wakiokolewa kutoka kwenye chombo cha majini {Ferry/kivuko} cha abiria cha Indonesia kilichokumbwa na matatizo katika Bahari ya Java, kulingana na shirika la Indonesia la utafutaji na uokoaji.

    Operesheni ya utafutaji na uokoaji ilianzishwa baada ya mawasiliano kupotea na meli ya {Virgo Transport 8}, iliyokuwa na watu 243, wakati ilipokumbana na hali mbaya ya hewa, shirika hilo lilisema.

    Shughuli za kuwatafuta abiria waliosalia zinaendelea.

    Kivuko hicho kilikuwa kikisafiri kutoka Surabaya kuelekea mji wa Banjarmasin katika eneo la Kalimantan Kusini, na taarifa za mwisho zilionyesha kuwa kilikuwa umbali wa takriban kilomita 150 (maili 93) kusini mwa Banjarmasin majira ya saa 02:00 asubuhi kwa saa za eneo hilo siku ya Jumapili (saa 18:00 GMT siku ya Jumamosi).

    Mamlaka zilipokea taarifa ya awali ya dharura saa 04:10 kutoka kwa kampuni inayoendesha meli hiyo, PT Virgo. Meli hiyo iliondoka Surabaya saa 10:33 siku ya Jumamosi na ilitarajiwa kuwasili Banjarmasin siku ya Jumapili saa 14:00, kulingana na taarifa kutoka tovuti mbili zinazofuatilia usafiri wa baharini.

    Kikosi kazi cha pamoja kinachohusisha shirika la Indonesia la utafutaji na uokoaji, jeshi la wanamaji, polisi wa majini na wadau wengine kimeundwa kwa ajili ya shughuli hiyo ya uokoaji.

    Meli na helikopta zimetumwa eneo la tukio, huku wafanyakazi 280 wakishiriki katika operesheni hiyo ya uokoaji. Meli zote zilizopo katika eneo la Bahari ya Java zimearifiwa kuripoti dalili zozote za kuwepo kwa abiria.

    Kituo cha uendeshaji kwa ajili ya kushughulikia ajali hiyo kilianzishwa katika eneo la Bandari ya Trisakti siku ya Jumapili asubuhi.

    Kuna abiria 213 na wafanyakazi 30 wa meli hiyo. Kati yao, watu 130 bado hawajulikani walipo.

    Rusmilawati, mkazi wa Banjarmasin, alienda bandarini kutafuta taarifa kuhusu ndugu zake wanane waliokuwa abiria kwenye meli hiyo. Walikuwa wakirejea Banjarmasin baada ya kutembelea makaburi ya wanazuoni kadhaa wa Kiislamu huko Java.

    "Awali walisafiri kwa ndege kwenda huko, lakini kwa safari ya kurudi walitaka kujaribu kusafiri kwa meli," aliambia BBC Indonesia.

    Kufikia alasiri ya Jumapili kwa saa za huko, Rusmilawati alisema hakuwa amepata taarifa yoyote kutoka kwa maafisa kuhusu iwapo ndugu zake walikuwa wameokolewa.

  2. Senegal ipo tayari kwa michezo ya Olimpiki ya vijana 2026

    Mwenge wa Michezo ya Olimpiki ya Vijana umewasili nchini Senegal kwa ajili ya safari ya kuuzungusha nchi nzima.

    Hii itakuwa mara ya kwanza kwa taifa hilo la Afrika Magharibi kuwa mwenyeji wa mashindano ya Olimpiki yatakayofanyika katika ardhi ya Afrika.

    Mwenge huo ulipokelewa katika mji mkuu wa Senegal baada ya kuwashwa katika Uwanja wa kihistoria wa Panathenaic jijini Athens, Ugiriki, Alhamisi iliyopita.

    Michezo ya Olimpiki ya Vijana itafanyika kuanzia tarehe 31 Oktoba hadi 13 Novemba katika maeneo ya Dakar, Diamniadio na Saly, huku takriban wanariadha 2,700 wakitarajiwa kushiriki katika michezo 25 tofauti.

    Tukio hili litakuwa hatua muhimu ya kihistoria kwa Senegal na bara zima, huku sherehe zikiwakutanisha vijana, wanariadha, wadau wa utamaduni, na viongozi wa jamii katika hafla ya kuhesabu siku zilizosalia iliyofanyika Dakar siku ya Jumamosi.

    Rais wa Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki (IOC), Kirsty Coventry kutoka Zimbabwe, alihudhuria hafla hiyo katika eneo la Place du Souvenir jijini Dakar, ambapo mwenge huo uliwashwa.

    Coventry, ambaye ni Mwafrika wa kwanza na mwanamke wa kwanza kuongoza IOC, alielezea Michezo hiyo kama fursa ya kuleta athari ya kudumu kwa vijana kote barani.

    "Lengo ni kwamba haitaleta athari kwa vijana wanaokuja hapa pekee, bali wanaporejea nyumbani, watazungumzia maadili na hamasa iliyotokana na Michezo hiyo ndani yao," alisema Coventry.

    Aliongeza kuwa safari ya mwenge huo nchini Senegal itasaidia kuongeza uelewa kuhusu tukio hilo muhimu na kuhamasisha jamii kote nchini.

    Mwenge huo utapita katika mikoa 14 ya Senegal kama sehemu ya ziara iliyolenga kuleta roho ya Michezo hiyo karibu na jamii za wenyeji kabla ya kurejea Dakar kwa ajili ya sherehe ya ufunguzi mwezi ujao.

    Michezo ya Dakar 2026 imesifiwa sana kama wakati muhimu kwa michezo barani Afrika, ikitoa jukwaa lisilo na kifani la kuonyesha vipaji vya vijana, utamaduni, na uwezo wa kuandaa matukio makubwa barani humo.

    Waandaaji wanatumai kuwa Michezo hiyo itaacha alama katika nyanja za maendeleo ya vijana, elimu, na ushiriki katika michezo, huku ikiimarisha nafasi inayokua ya Afrika katika harakati za kimataifa za Olimpiki.

  3. Akili unde yatishia maisha ya binadamu, wasema wataalamu

    Mtafiti wa akili bandia (AI) aliyeacha kazi katika kampuni ya Anthropic amesema kuwa watu wanaoshughulikia teknolojia hiyo walikuwa na "hofu" kuhusu kasi ya maendeleo yake na nini inaweza kumaanisha kwa wanadamu.

    Jacob Coxon alimweleza mwandishi wa BBC Laura Kuenssberg katika mahojiano kuhusu ujumbe wake wa kujiuzulu uliosambaa sana, ambapo alielezea wasiwasi wake kuhusu AI inayokwenda bila udhibiti.

    "Ninaamini kwamba tusipopunguza kasi ya maendeleo ya sasa, kuna uwezekano mkubwa kwamba sote tunaweza kupoteza maisha katika siku za usoni," alisema.

    Hatua yake ya kujiuzulu inakuja wakati kukiwa na wasiwasi unaoongezeka kuhusu usalama katika sekta hiyo, ikiwa ni pamoja na maoni kutoka kwa bosi wake wa zamani, mkuu wa Anthropic Dario Amodei, ambaye katika makala alitetea wazo la kupunguza kasi ya maendeleo.

    Viongozi wa kampuni mbili pinzani za AI, Sam Altman wa OpenAI na Elon Musk wa xAI, wote wamesema wanaunga mkono pendekezo la Amodei la kupunguza kasi na kuweka udhibiti katika sekta nzima, pamoja na ufuatiliaji huru wa uundaji wa mifumo ya AI.

    Amodei alisema kuwa suala la kuendeleza teknolojia hiyo halina shaka, lakini hatari zinazohusiana nayo ni "kubwa", na kwamba makampuni pamoja na serikali lazima vipewe muda wa kushughulikia changamoto hizo.

    Coxon, mwenye umri wa miaka 27—ambaye aliwahi kufanya kazi OpenAI kabla ya kujiunga na Anthropic—aliunga mkono wazo la kupunguza kasi lakini akasema hatua hiyo inahitaji kuratibiwa na China ili kuepuka "mashindano ya kimataifa".

    Kulingana na Coxon, swali gumu zaidi kujibu lilikuwa ni jinsi maangamizi yanayosababishwa na Akili Bandia (AI) yangeonekana.

    Moja ya hatari zilizotajwa katika maoni ya Amodei ilikuwa ni uwezekano wa kundi la programu-roboti (bots) kufanya kazi kama kompyuta kuu yenye nguvu (supercomputer) na kuweza kutawala mtandao.

    Coxon alisema hali hii inaweza kuwa halisi ndani ya kipindi cha miezi sita hadi mwaka mmoja.

    Kufuatia kuondoka kwa Coxon, msemaji wa kampuni ya Anthropic aliambia BBC News: "Siku zote tumekuwa wazi kwamba AI italeta faida kubwa na pia hatari ambazo hazijawahi kushuhudiwa.

    Wadau wa sekta hiyo wamependekeza kuwa maoni kuhusu hatari na nguvu ya AI huenda yanalenga tu kuzua gumzo au taharuki. Wakosoaji wengine wanasema Anthropic imekuwa ikijaribu kuchochea hatua za udhibiti ili kuzuia ushindani, na hivyo kuiacha yenyewe na OpenAI zikitawala soko pekee (duopoly).

    Inaripotiwa kuwa Anthropic inajiandaa kwa hatua ya kuuza hisa zake kwa umma kwa mara ya kwanza (IPO), hatua ambayo inaweza kuweka rekodi mpya.

    OpenAI ilitarajiwa kufanya vivyo hivyo, lakini Altman alisema kuwa huo ungekuwa "wakati usiofaa" kufanya hivyo "kutokana na hali ya sasa kuhusu masuala ya usalama," katika mahojiano na jarida la Fortune siku ya Ijumaa.

    Hata hivyo, Coxon alikuwa na matumaini fulani kuhusu mustakabali wa AI, akiambia BBC kuwa watu wanaofanya utafiti wa teknolojia hiyo "kwa dhati wanataka kuona matokeo chanya" ya mambo kama vile "kutatua matatizo ya magonjwa na kuboresha maisha ya kila mtu".

    Kauli zake kuhusu AI zimesambazwa mara mamilioni kwenye mitandao ya kijamii, huku mwanasayansi wa Anthropic, Evan Hubinger, akijibu kwenye mtandao wa X kwamba anakubaliana na Coxon.

    "Kwa kweli tunaamini kabisa kuwa AI inaweza kuua wanadamu wote! Binafsi nadhani kuna uwezekano wa zaidi ya asilimia 10 (10%) ndani ya muongo ujao," alisema Hubinger.

    Watu mashuhuri katika nyanja ya AI wamekuwa wakitoa tahadhari kuhusu tishio la kiusalama linaloletwa na teknolojia hiyo kwa miaka mingi sasa, huku viongozi wa OpenAI, Google DeepMind, na Anthropic wakieleza hayo mwaka wa 2023.

    Tahadhari hizi zimezidi kusikika kwa nguvu katika wiki za hivi karibuni, kadiri mifumo mipya inavyoonyesha uwezo mkubwa zaidi ambao huenda wabunifu wake wanapata changamoto kuudhibiti.

    Mwezi Aprili, Anthropic ilisema kuwa inazuia mfumo wake wa 'Mythos' kutumiwa na umma kwa sababu unaweza kujiondoa wenyewe kutoka kwenye mazingira ya majaribio, yanayojulikana kama 'sandbox'.

    OpenAI pia imesema kuwa baadhi ya hatua katika uundaji wa mfumo wake wa hivi karibuni wa 'Astra' zimesitishwa, ikitaja wasiwasi kuhusu usalama wa mtandaoni.

  4. Uganda yaamrisha wanafunzi kutoka DRC kuwekwa karantini kwa siku 21 kabla ya kurejea shuleni

    Serikali ya Uganda imeamuru wanafunzi wanaosafiri kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kukaa karantini kwa lazima kwa siku 21 wakati muhula mpya wa masomo ukianza.

    Wanafunzi wanaowasili kutoka DRC lazima wakamilishe kipindi cha siku 21 cha karantini, muda ambao unaendana na kipindi cha maambukizi ya virusi vya Ebola kabla ya dalili kujitokeza.

    Katibu wa Kudumu katika Wizara ya Elimu, Dkt. Kedrace Turyagyenda, amesema agizo hilo limetolewa kufuatia tathmini ya kitaalamu ya hatari na kubainisha kuwa wanafunzi hao waliowekwa karantini watafuatiliwa kwa karibu kabla ya kuripoti katika shule zao husika.

    Agizo hilo limetolewa wakati shule zikijiandaa kufunguliwa kwa ajili ya muhula wa tatu.

    Hatua hiyo ni sehemu ya itifaki na tahadhari za kiafya zinazoendelea kutekelezwa katika eneo hilo kufuatia milipuko ya Ebola katika baadhi ya maeneo ya DRC.

    Uganda ilitangazwa kuwa haina maambukizi ya Ebola mnamo tarehe 26 Agosti 2026, baada ya kukamilisha kipindi cha lazima cha ufuatiliaji cha siku 42 kufuatia mgonjwa wa mwisho kuruhusiwa kutoka hospitalini mnamo tarehe 16 Julai 2026.

    Wakati huo huo nchini DRC, mlipuko wa Ebola unaosababishwa na virusi vya Bundibugyo umeenea hadi eneo jipya la huduma za afya, na kufanya idadi ya walioathirika kufikia 61 katika mikoa sita kati ya mikoa 26 ya nchi hiyo, Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema Alhamisi.

    Katika taarifa yake ya hivi karibuni, WHO ilisema mlipuko huo umeenea hadi eneo la huduma za afya la Kayna katika mkoa wa Kivu Kaskazini tangu taarifa yake ya tarehe 28 Agosti.

    Kufikia Septemba 7, nchi hiyo ilikuwa imeripoti visa 6,757 vilivyothibitishwa, ikiwa ni pamoja na vifo 3,267, na kusababisha uwiano wa vifo vya wagonjwa wa 48.3%.

    Mlipuko huo unaathiri maeneo ya afya katika majimbo ya Bas-Uele, Haut-Uele, Ituri, Kivu Kaskazini, Kivu Kusini na Tshopo.

    WHO ilisema mienendo ya maambukizi inabaki kuwa tofauti katika maeneo yaliyoathiriwa, huku kukiwa na ushahidi wa upanuzi unaoendelea wa kijiografia na ongezeko endelevu la visa katika baadhi ya maeneo ya afya.

  5. Homa ya nguruwe yawaua nguruwe 1500 Kenya

    Serikali ya Kenya imeongeza juhudi za kudhibiti mlipuko wa Homa ya Nguruwe ambayoimeua karibu nguruwe 1,500 katika mashamba zaidi ya 20 katika Kaunti ya Kiambu tangu Mei.

    Idara ya Huduma za Mifugo inasema ugonjwa huo pia umeripotiwa katika kaunti zingine sita: Tharaka-Nithi, Embu, Kakamega, Busia, Homa Bay, na Migori ambapo visa na vifo zaidi vimerekodiwa.

    Mlipuko huo umesababisha ufuatiliaji ulioimarishwa na hatua za kuzuia kuenea zaidi katika mipaka ikiwa ni pamoja na kuzuia uhamaji wa mifugo.

    Takriban nguruwe 1,470 hadi 1,500 wamekufa Kiambu pekee, na kuwaathiri wakulima wa eneo hilo vikali na kutishia maisha.

    Mamlaka inasisitiza kwamba Homa ya Nguruwe ya Afrika ni ugonjwa unaoambukiza unaoathiri nguruwe wa kufugwa na wa porini, lakini hauambukizi binadamu.

    Idara ya Huduma za Mifugo (DVS) imeongeza ufuatiliaji, na udhibiti wa uhamaji wa mifugo kote nchini.

    Serikali za kaunti na mamlaka za kilimo zimepuuzilia mbalia taarifa ambazo zimezitaja kama uvumi unaodai kwamba Shirika la Utafiti wa Kilimo na Mifugo la Kenya (KALRO) lilisambaza watoto wa nguruwe walioambukizwa.

  6. Tetesi: Arsenal kushindana na Real Madrid katika kumsajili Nico Paz

    Arsenal inamfuatilia Nico Paz, Liverpool na Aston Villa zinamtazama Cher Ndour, na Sunderland haitaki kukata tamaa katika juhudi za kumsajili Geny Catamo.

    Arsenal inafuatilia maendeleo ya mshambuliaji wa Argentina anayechezea Como, Nico Paz (22), lakini Real Madrid ina haki ya kumnunua tena kwa euro milioni 80 (pauni milioni 68.7). (ElDesmarque – In Spanish)

    Liverpool na Aston Villa ni miongoni mwa klabu zinazomfuatilia kiungo wa kati wa Italia anayechezea Fiorentina, Cher Ndour (22). (Caught Offside)

    Sunderland haitaki kukata tamaa katika juhudi za kumsajili Geny Catamo kutoka Sporting baada ya kushindwa kumnunua winga huyo wa Msumbiji (25) wakati wa dirisha la usajili la majira ya joto. (Record, via Sport Witness)

    Monaco inaamini inaweza kupata euro milioni 70 (pauni milioni 60.1) kwa ajili ya Lamine Camara kiungo wa kati wa Senegal mwenye umri wa miaka 22 anayewaniwa na Chelsea na Liverpool ambaye uhamisho wake kwenda Stamford Bridge ulikwama katika siku ya mwisho ya dirisha la usajili. (TeamTalk)

    Mshambuliaji wa Ujerumani, Lukas Nmecha (25), anatarajia kuondoka Leeds United mkataba wake utakapomalizika mwishoni mwa msimu huu iwapo hatapata muda wa kutosha kucheza. (Football Insider)

    Celtic inamfuatilia beki wa kushoto wa England anayechezea Liverpool, Luke Chambers (22), huku ikitathmini uwezekano wa kumsajili katika dirisha la usajili la mwezi Januari. (Football Insider)

    Winga wa Ivory Coast, Wilfried Zaha (33), amependekezwa kwa klabu ya Malaga baada ya kuondoka Galatasaray kama mchezaji huru kufuatia vipindi viwili vya mkopo katika timu ya MLS, Charlotte FC. (Mundo Deportivo – In Spanish)

    Raphinha ana mkataba na Barcelona hadi mwaka 2028, lakini mabingwa hao wa Uhispania tayari wanatafakari kumpa winga huyo wa Brazil (29) nyongeza ya mkataba hadi mwaka 2030. (AS – In Spanish)

    Pia, Barca imekamilisha makubaliano ya kuongeza mkataba wa mshambuliaji wa Misri mwenye umri wa miaka 18, Hamza Abdelkarim, hadi mwaka 2030, ikiwa na kipengele cha bei ya kuvunja mkataba cha euro milioni 150 (pauni milioni 128.7). (Sport – In Spanish)

    Arsenal na Chelsea zinaongoza katika mbio za kumsajili winga wa Norway mwenye umri wa miaka 15 anayechezea Valerenga, Gabriel Rajkovic. (TeamTalk)

  7. Vuguvugu la kisiasa nchini Kenya Linda mwanachi lazuru Nairobi

    Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna anakabiliwa na kibarua kigumu cha kisiasa Jumapili hii anapojiandaa kupima umaarufu wake katika kaunti anayoiwakilisha katika Bunge la Seneti la Nairobi kwa kuandaa mkutano mkubwa wa kisiasa.

    Muungano wa kiaissa wa Linda Mwananchi unapeleka kampeni yake mjini Nairobi katika ziara kuu ya uhamasishaji inayotarajiwa kuhitimishwa kwa mkutano mkubwa katika Uwanja wa Jacaranda ambao ulikuwa maarufu na mojawapo ya ngome za kisasa za kinara wa zamani wa ODM Raila Odinga.

    Ziara hiyo ya Nairobi inayosubiriwa kwa hamu imeanza katika Kanisa Kuu la All Saints ambapo kundi hilo lilifika saa tatu asubuhi kuhudhuria ibada ya Jumapili, kabla ya vuguvugu hilo kuanza ziara katika baadhi ya masoko na maeneo yenye shughuli nyingi jijini.

    Polisi wameshika doria katika maeneo mbalimbali Jijini Nairobi hasa Katikati mwa Jiji na kwenye barabara kuu za Outering na Jogoo na vile vile katika uwanja huo wa Jacaranda.

    Kutoka kanisani, Sifuna na wafuasi wake wanatarajiwa kuelekea masoko ya Marikiti na Gikomba kabla ya kuendelea hadi Soko la Burma.

    Ratiba hiyo kisha italipeleka vuguvugu hilo katika maeneo ya Stage 17, B Centre na Manyanja, ikifuatiwa na maandamano kando ya Barabara ya Jogoo.

    Ziara hiyo imepangwa kuhitimishwa katika Uwanja wa Jacaranda mwendo wa saa nane mchana, ambapo Sifuna anatarajiwa kuhutubia mkutano mkubwa.

    Harakati hizi za uhamasishaji jijini Nairobi zinafanyika wakati seneta huyo akijaribu kupanua wigo wa Linda vuguvugu la Mwananchi nje ya msingi wake wa uungwaji mkono unaokua, na kuonyesha kuwa vuguvugu hilo linaweza kuvutia wafuasi wengi wa kisiasa jijini.

    Sifuna amewahimiza wafuasi wake kujitokeza kwa wingi katika tukio ambalo washirika wake tayari wamelielezea kama "mama wa mikutano yote" .

    Katika ujumbe ulioshirikiwa kwenye mitandao ya kijamii, Sifuna aliwasilisha ratiba ya Jumapili kama mchanganyiko wa maombi na uhamasishaji wa kisiasa, akiwataka wafuasi kutokuwa na visingizio vya kutohudhuria.

  8. Wahouthi watangaza mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani dhidi ya kambi ya kijeshi ya Saudia

    Kundi la Houthi la Yemen limetangaza kuwa limeishambulia kambi ya kijeshi kusini mwa Saudi Arabia kwa kutumia makombora ya balistiki na ndege zisizo na rubani.

    Yahya Saree, msemaji wa kijeshi wa kundi la Houthi, aliandika kwenye mtandao wa kijamii wa X kwamba shambulio hilo lililenga kambi ya Sharura iliyoko kusini mwa Saudi Arabia.

    Kwa mujibu wake, mashambulizi hayo yalilenga "ghala za silaha pamoja na vituo vya amri na udhibiti" vya Saudi Arabia.

    Bw. Saree hakutaja muda kamili wa shambulio hilo, lakini alionya kuwa kuendelea kwa hatua za kijeshi dhidi ya Yemen kungesababisha mashambulizi makali zaidi na mapana yatakayofika ndani kabisa ya ardhi ya Saudi Arabia.

  9. IRGC yaonya dhidi ya meli za Marekani zinazokaribia mlango wa Hormuz

    Ali Mohammadi, naibu afisa wa masuala ya kisiasa katika Jeshi la Wanamaji la Walinzi wa Mapinduzi (IRGC), akirejelea kauli za Rais wa Marekani Donald Trump kuhusu kudhibiti wa Lango la Hormuz, alisema: "Ikiwa ndivyo ilivyo, kwa jina la Mungu, leteni mojawapo ya meli zenu ndani ya umbali wa kilomita 100."

    Afisa huyo mwandamizi wa IRGC alisema: "Wamarekani wanajua kuwa iwapo meli zao zitakaribia, zitakabiliwa na jibu kutoka kwa vikosi vya Iran," na bila kutoa maelezo zaidi, alidai kuwa "mfano wa tukio kama hilo umeshuhudiwa pia katika siku za hivi karibuni."

    Akizungumza katika mkutano wa usiku wa wafuasi wa serikali mjini Mashhad, alisema: "Leo... hakuna wanajeshi wa Marekani katika Ghuba ya Uajemi, Bahari ya Oman, na Lango la Hormuz, wala hakuna vifaa vya Marekani vilivyowekwa katika maeneo hayo. Iwapo Wamarekani watakaribia eneo hilo lililozuiliwa, wao wenyewe wanajua nini kitawapata."

    Kulingana na yeye, "Meli yoyote inayotoka Kuwait na Bahrain, bila ubaguzi, huwa chini ya uangalizi wa Jeshi la Wanamaji la IRGC, na iwapo ukiukwaji wowote utabainika, hatua zitachukuliwa kwa mujibu wa kanuni zilizowekwa."

  10. Natumai hujambo na karibu katika habari zetu za moja kwa moja