6 wafariki, 107 waokolewa kwenya ajali ya kivuko huko Java, Indonesia
Watu sita wamefariki dunia huku wengine 107 wakiokolewa kutoka kwenye chombo cha majini {Ferry/kivuko} cha abiria cha Indonesia kilichokumbwa na matatizo katika Bahari ya Java, kulingana na shirika la Indonesia la utafutaji na uokoaji.
Operesheni ya utafutaji na uokoaji ilianzishwa baada ya mawasiliano kupotea na meli ya {Virgo Transport 8}, iliyokuwa na watu 243, wakati ilipokumbana na hali mbaya ya hewa, shirika hilo lilisema.
Shughuli za kuwatafuta abiria waliosalia zinaendelea.
Kivuko hicho kilikuwa kikisafiri kutoka Surabaya kuelekea mji wa Banjarmasin katika eneo la Kalimantan Kusini, na taarifa za mwisho zilionyesha kuwa kilikuwa umbali wa takriban kilomita 150 (maili 93) kusini mwa Banjarmasin majira ya saa 02:00 asubuhi kwa saa za eneo hilo siku ya Jumapili (saa 18:00 GMT siku ya Jumamosi).
Mamlaka zilipokea taarifa ya awali ya dharura saa 04:10 kutoka kwa kampuni inayoendesha meli hiyo, PT Virgo. Meli hiyo iliondoka Surabaya saa 10:33 siku ya Jumamosi na ilitarajiwa kuwasili Banjarmasin siku ya Jumapili saa 14:00, kulingana na taarifa kutoka tovuti mbili zinazofuatilia usafiri wa baharini.
Kikosi kazi cha pamoja kinachohusisha shirika la Indonesia la utafutaji na uokoaji, jeshi la wanamaji, polisi wa majini na wadau wengine kimeundwa kwa ajili ya shughuli hiyo ya uokoaji.
Meli na helikopta zimetumwa eneo la tukio, huku wafanyakazi 280 wakishiriki katika operesheni hiyo ya uokoaji. Meli zote zilizopo katika eneo la Bahari ya Java zimearifiwa kuripoti dalili zozote za kuwepo kwa abiria.
Kituo cha uendeshaji kwa ajili ya kushughulikia ajali hiyo kilianzishwa katika eneo la Bandari ya Trisakti siku ya Jumapili asubuhi.
Kuna abiria 213 na wafanyakazi 30 wa meli hiyo. Kati yao, watu 130 bado hawajulikani walipo.
Rusmilawati, mkazi wa Banjarmasin, alienda bandarini kutafuta taarifa kuhusu ndugu zake wanane waliokuwa abiria kwenye meli hiyo. Walikuwa wakirejea Banjarmasin baada ya kutembelea makaburi ya wanazuoni kadhaa wa Kiislamu huko Java.
"Awali walisafiri kwa ndege kwenda huko, lakini kwa safari ya kurudi walitaka kujaribu kusafiri kwa meli," aliambia BBC Indonesia.
Kufikia alasiri ya Jumapili kwa saa za huko, Rusmilawati alisema hakuwa amepata taarifa yoyote kutoka kwa maafisa kuhusu iwapo ndugu zake walikuwa wameokolewa.