Akili unde yatishia maisha ya binadamu, wasema wataalamu

Chanzo cha picha, Getty Images
Mtafiti wa akili bandia (AI) aliyeacha kazi katika kampuni ya Anthropic amesema kuwa watu wanaoshughulikia teknolojia hiyo walikuwa na "hofu" kuhusu kasi ya maendeleo yake na nini inaweza kumaanisha kwa wanadamu.
Jacob Coxon alimweleza mwandishi wa BBC Laura Kuenssberg katika mahojiano kuhusu ujumbe wake wa kujiuzulu uliosambaa sana, ambapo alielezea wasiwasi wake kuhusu AI inayokwenda bila udhibiti.
"Ninaamini kwamba tusipopunguza kasi ya maendeleo ya sasa, kuna uwezekano mkubwa kwamba sote tunaweza kupoteza maisha katika siku za usoni," alisema.
Hatua yake ya kujiuzulu inakuja wakati kukiwa na wasiwasi unaoongezeka kuhusu usalama katika sekta hiyo, ikiwa ni pamoja na maoni kutoka kwa bosi wake wa zamani, mkuu wa Anthropic Dario Amodei, ambaye katika makala alitetea wazo la kupunguza kasi ya maendeleo.
Viongozi wa kampuni mbili pinzani za AI, Sam Altman wa OpenAI na Elon Musk wa xAI, wote wamesema wanaunga mkono pendekezo la Amodei la kupunguza kasi na kuweka udhibiti katika sekta nzima, pamoja na ufuatiliaji huru wa uundaji wa mifumo ya AI.
Amodei alisema kuwa suala la kuendeleza teknolojia hiyo halina shaka, lakini hatari zinazohusiana nayo ni "kubwa", na kwamba makampuni pamoja na serikali lazima vipewe muda wa kushughulikia changamoto hizo.
Coxon, mwenye umri wa miaka 27—ambaye aliwahi kufanya kazi OpenAI kabla ya kujiunga na Anthropic—aliunga mkono wazo la kupunguza kasi lakini akasema hatua hiyo inahitaji kuratibiwa na China ili kuepuka "mashindano ya kimataifa".
Kulingana na Coxon, swali gumu zaidi kujibu lilikuwa ni jinsi maangamizi yanayosababishwa na Akili Bandia (AI) yangeonekana.
Moja ya hatari zilizotajwa katika maoni ya Amodei ilikuwa ni uwezekano wa kundi la programu-roboti (bots) kufanya kazi kama kompyuta kuu yenye nguvu (supercomputer) na kuweza kutawala mtandao.
Coxon alisema hali hii inaweza kuwa halisi ndani ya kipindi cha miezi sita hadi mwaka mmoja.
Kufuatia kuondoka kwa Coxon, msemaji wa kampuni ya Anthropic aliambia BBC News: "Siku zote tumekuwa wazi kwamba AI italeta faida kubwa na pia hatari ambazo hazijawahi kushuhudiwa.
Wadau wa sekta hiyo wamependekeza kuwa maoni kuhusu hatari na nguvu ya AI huenda yanalenga tu kuzua gumzo au taharuki. Wakosoaji wengine wanasema Anthropic imekuwa ikijaribu kuchochea hatua za udhibiti ili kuzuia ushindani, na hivyo kuiacha yenyewe na OpenAI zikitawala soko pekee (duopoly).
Inaripotiwa kuwa Anthropic inajiandaa kwa hatua ya kuuza hisa zake kwa umma kwa mara ya kwanza (IPO), hatua ambayo inaweza kuweka rekodi mpya.
OpenAI ilitarajiwa kufanya vivyo hivyo, lakini Altman alisema kuwa huo ungekuwa "wakati usiofaa" kufanya hivyo "kutokana na hali ya sasa kuhusu masuala ya usalama," katika mahojiano na jarida la Fortune siku ya Ijumaa.
Hata hivyo, Coxon alikuwa na matumaini fulani kuhusu mustakabali wa AI, akiambia BBC kuwa watu wanaofanya utafiti wa teknolojia hiyo "kwa dhati wanataka kuona matokeo chanya" ya mambo kama vile "kutatua matatizo ya magonjwa na kuboresha maisha ya kila mtu".
Kauli zake kuhusu AI zimesambazwa mara mamilioni kwenye mitandao ya kijamii, huku mwanasayansi wa Anthropic, Evan Hubinger, akijibu kwenye mtandao wa X kwamba anakubaliana na Coxon.
"Kwa kweli tunaamini kabisa kuwa AI inaweza kuua wanadamu wote! Binafsi nadhani kuna uwezekano wa zaidi ya asilimia 10 (10%) ndani ya muongo ujao," alisema Hubinger.
Watu mashuhuri katika nyanja ya AI wamekuwa wakitoa tahadhari kuhusu tishio la kiusalama linaloletwa na teknolojia hiyo kwa miaka mingi sasa, huku viongozi wa OpenAI, Google DeepMind, na Anthropic wakieleza hayo mwaka wa 2023.
Tahadhari hizi zimezidi kusikika kwa nguvu katika wiki za hivi karibuni, kadiri mifumo mipya inavyoonyesha uwezo mkubwa zaidi ambao huenda wabunifu wake wanapata changamoto kuudhibiti.
Mwezi Aprili, Anthropic ilisema kuwa inazuia mfumo wake wa 'Mythos' kutumiwa na umma kwa sababu unaweza kujiondoa wenyewe kutoka kwenye mazingira ya majaribio, yanayojulikana kama 'sandbox'.
OpenAI pia imesema kuwa baadhi ya hatua katika uundaji wa mfumo wake wa hivi karibuni wa 'Astra' zimesitishwa, ikitaja wasiwasi kuhusu usalama wa mtandaoni.




