Trump asema Marekani itaudhibiti kijeshi Mlango-Bahari wa Hormuz
Rais wa Marekani Donald Trump amesema Marekani itaweka “kizuizi cha kijeshi” na kuudhibiti Mlango Bahari wa Hormuz, njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta duniani, kufuatia kushindwa kwa mazungumzo kati ya Marekani na Iran.
Trump amesema kupitia ujumbe wake katika mtandao wa Truth Social kuwa Jeshi la Wanamaji la Marekani litachukua hatua hiyo baada ya mazungumzo ya ngazi ya juu yaliyofanyika Islamabad, Pakistan, kushindwa kufikia makubaliano pamoja na mambo mengine, kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran.
Ameongeza kuwa mazungumzo hayo yalivunjika kwa sababu Iran “haiko tayari kuachana na malengo yake ya nyuklia,” akisisitiza kuwa Washington ilihudhuria mazungumzo hayo kwa nia ya kutafuta suluhu ya kudumu.
Hatua hiyo inakuja wakati mvutano kati ya Marekani na Iran ukiendelea kuongezeka, huku juhudi za kidiplomasia za muda mrefu zikishindwa mara kadhaa kufanikisha makubaliano kuhusu mpango wa nyuklia wa Tehran.
Mlango Bahari wa Hormuz ni njia muhimu ya kimkakati inayopitisha sehemu kubwa ya mafuta ya dunia kutoka Mashariki ya Kati, na hatua ya Marekani inaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa masoko ya nishati na usafirishaji wa kimataifa.