Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Mjumbe wa Trump, Waziri wa Iran waelekea Uswizi kwa mazungumzo

Israel na Hezbollah walikubaliana kusitisha mapigano nchini Lebanon siku ya Ijumaa ambayo ni muhimu kwa ajili ya kufunguliwa tena kwa Mlango-Bahari wa Hormuz.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Almirón anaswa na jinamizi la VAR

    Miguel Almirón amekuwa mchezaji wa kwanza kuadhibiwa kwa kadi nyekundu baada ya kufunika mdomo wake katika Kombe la Dunia, huku Paraguay wakibaki na matumaini ya kusonga mbele licha ya kucheza wachezaji 10 na kuiondoa Uturuki dimbani.

    Paraguay walianza kwa kasi baada ya dakika 64 tu kupitia bao la haraka lililofungwa na Matías Galarza, na likawa bao la ushindi katika mechi hiyo. Hata hivyo, Uturuki walitawala mchezo kwa muda mwingi wakitafuta kusawazisha.

    Mvutano uliongezeka kabla ya mapumziko Almirón alipoweka mkono wake kufunika mdomo katika mzozo na Mert Müldür, hatua iliyosababisha VAR kuingilia kati na mwamuzi Iván Barton kumtoa nje kwa kadi nyekundu kutokana na sheria mpya ya FIFA ya udhibiti wa mawasiliano uwanjani.

    Timu zote mbili zilikuwa zimepoteza, Paraguay ikifungwa 4-1 na wenyeji Marekani, huku Australia ikiichapa Uturuki 2-0. Hii ilifanya mchezo huu uwe wa ushindani mkubwa na shinikizo, kwani kila timu ilikuwa inahitaji ushindi.

    Uturuki walitawala mchezo kwa kiasi kikubwa, lakini walikosa umakini wa kumalizia wa kumaliza kwa kishindo. Walipiga mashuti 12, lakini ni moja tu lililolenga lango. Pia walikaribia kufunga kupitia mpira wa kichwa wa Muldur uliogonga mwamba na lango.

    Baada ya mapumziko, Demiral alijaribu kumtisha kipa wa Paraguay, Orlando Gill, lakini hakuweza kumfunga. Mchezaji wa akiba Deniz Gul alipata nafasi nzuri ya kufunga kwa kichwa karibu na lango lakini akapiga moja kwa moja kwa kipa.

    Soma zaidi:

  2. Rais wa Bolivia atangaza hali ya dharura huku mzozo wa kiuchumi ukizidi

    Rais wa Bolivia Rodrigo Paz ametangaza hali ya dharura katika taifa hilo la Marekani Kusini huku mzozo na waandamanaji ukiendelea kwa zaidi ya siku 50.

    Hatua hii itatoa nafasi ya kupelekwa kwa wanajeshi zaidi ili kurejesha utulivu na kuondoa vizuizi vilivyowekwa na waandamanaji.

    Makundi ya waandamanaji ambayo mengi yanamuunga mkono Rais wa zamani wa mrengo wa kushoto Evo Morales yamefunga barabara kuu, hatua ambayo imekatiza usafiri wa malori na hivyo kuzuia usambazaji wa chakula, mafuta na madawa katika maeneo mengi, ikiwa ni pamoja na mji muhimu wa La Paz.

    Mzozo wa sasa ulianza baada ya rais Paz kukata kwa ghafla ruzuku ya mafuta iliyokuwepo kwa muda mrefu, huku sarafu ikishuka thamani na taifa kuanza mazungumzo na shirika la kimataifa la fedha IMF.

    Licha ya hatua za kupunguza bei ya mafuta na kusimamisha mageuzi ya mfumo wa ardhi ambayo hayakupendelewa na wengi, maandamano yaliongezeka huku vyama vya wafanyakazi vikidai nyongeza ya mishahara, na kumtaka Paz ajiuzulu.

    Tangazo la hivi punde la Paz limetokea saa chache tu baada ya kusaini makubaliano na chama kikuu cha wafanyakazi wa Bolivia (COB) ambayo yalilenga kupunguza mvutano.

    Paz alisema hali ya dharura inalenga kurudisha utulivu, kulinda raia na kuhakikisha usambazaji wa bidhaa muhimu, huku akionya kwamba wanaoendeleza usumbufu watakabiliwa na mkono wa kisheria.

  3. Kombe la dunia 2026: Kanuni mpya za FIFA zatikisa hesabu za kufuzu

    Kumekuwa na mabadiliko madogo lakini muhimu katika jinsi FIFA inavyopanga makundi kwenye Kombe la Dunia la 2026, na huenda ikawa na athari kubwa kwenye mechi za mwisho za makundi.

    Kwa mara ya kwanza katika historia ya Kombe la Dunia, FIFA inatumia rekodi ya matokeo yote kama kigezo cha kwanza cha kutenganisha timu zilizo na idadi sawa ya pointi, badala ya kutumia tofauti ya mabao.

    Athari za mfumo mpya tayari zimeanza kuonekana huku Haiti na Uturuki zikiaga michuano mapema licha ya kutofautiana kwa pointi tatu pekee na timu zilizo mbele yao.

    Wenyeji wenza, Mexico na Marekani, kwa upande mwingine, tayari wamehakikisha kumaliza juu ya makundi yao wakiwa bado na mechi moja mkononi.

    "Kabla ya mwaka 1966, FIFA ilitumia mfumo wa uwiano wa mabao kuamua nafasi za timu zilizolingana kwa pointi. Mfumo huo ulizingatia mabao yaliyofungwa dhidi ya yaliyofungwa na timu husika.

    Mwaka 1970, FIFA ilianza kutumia mfumo wa tofauti ya mabao uliodumu hadi sasa.

    Hatua hii inaifanya FIFA kuendana na UEFA, ambayo kwa muda mrefu imekuwa ikitoa kipaumbele kwa matokeo ya moja kwa moja kati ya timu zinazolinganishwa.

    Sababu ya mfumo huu mpya ni kwamba unaangalia matokeo ya moja kwa moja kati ya timu mbili, jambo ambalo linaonekana kuwa la haki zaidi. Hii inaepusha athari za ushindi mkubwa usio wa kawaida, kama ule wa Ujerumani kuichapa Curaçao mabao 7-1.

    Hata hivyo, wengine wanaamini kuwa kutumia tofauti ya mabao ni bora zaidi kwa sababu hupima rekodi ya jumla ya timu katika kundi lote, badala ya kutegemea matokeo ya mechi moja tu kati ya timu husika.

    Soma zaidi:

  4. Trump azindua ndege ya kifahari iliyotolewa na Qatar kuwa Air Force One

    Rais Donald Trump amezindua ndege mpya aina ya Boeing 747-8 ya kutumiwa kwa safari za rais maarufu kama Air Force One ambayo ilitolewa kama zawadi "isiyokuwa na masharti" na serikali ya Qatar kwa Marekani mwaka jana.

    Jeshi la Marekani limekamilisha marekebisho ya ndege hiyo ya kifahari, ambayo imekadiriwa kuwa na thamani ya $400m (£300m).

    "Ndege hii iligeuzwa kuwa Ikulu ya White House katika kiwango cha kifahari ambacho hakuna mtu amewahi kukishuhudia," Trump alisema katika hotuba yake katika kituo cha Joint Base Andrews siku ya Ijumaa.

    Jeshi la wana anga la Marekani lilisema katika taarifa kwa vyombo vya habari kwamba ndege hiyo itaanza safari za majaribio ya mwisho, kabla ya kuanza kutumiwa kumsafirisha rais.

    Jeshi pia lilisema kuwa marekebisho ya ndege hiyo yalijumuisha uboreshaji wa mifumo ya usalama, mawasiliano na teknolojia, na kwamba waliondoa vitisho vyovyote vinavyowezekana kuwepo katika ndege hiyo.

    Mnamo Mei 2025, familia ya kifalme ya Qatar ilitoa zawadi ya ndege ya kifahari aina ya Boeing 747-8 kwa idara ya ulinzi ya Marekani ili itumike kama sehemu ya safu ya ndege zinazoitwa Air Force One, ambazo hutoa huduma za usafiri kwa rais.

    Wakati habari hizo zilipofichuliwa mwaka jana, zilizua mjadala kutoka pande zote mbili za kisiasa Marekani, wakiwemo baadhi ya washirika wa Trump. Wakosoaji waliteta kuwa kukubali mchango huo wa thamani ya juu kunaleta mgongano wa kimaslahi na huenda ni kinyume cha katiba.

    Ingawa sheria ya Marekani inaonyesha kwamba maafisa wa Marekani wanaweza tu kupokea zawadi chini ya $480, Ikulu ya White House imesisitiza kuwa kukubali ndege hiyo ni halali, na kuahidi kwamba itatolewa kama zawadi kwa maktaba ya rais Trump mara tu atakapoondoka madarakani.

    Kabla ya kuongezwa kwa ndege hiyo ya Qatar, safu ya Air Force One ilijumuisha ndege mbili za 747-200B ambazo zimekuwa zikitumika tangu 1990.

    Jeshi lilisema ndege hiyo mpya itatumiwa na rais kwa muda wa mpito hadi Boeing iwasilishe ndege zake mbili za VC-25B ambazo zimepangiwa kwa matumizi ya muda mrefu ya Air Force One, lakini kumekuwa na ucheleweshaji katika utengenezaji wake.

    Pia unaweza kusoma:

  5. Shuti kali la Saibari laihakikishia Morocco ushindi muhimu

    Morocco ilipata bao la mapema dhidi ya Scotland katika Uwanja wa Boston na haikuangalia nyuma tena. Bao pekee la Atlas Lions lilifungwa na Ismael Saibari, ambaye alipenya nyuma ya safu ya ulinzi ya Scotland, akautuliza mpira uliopigwa kwa ustadi na Brahim Diaz, kisha akaupiga kwa nguvu ukampita Angus Gunn na kutinga juu ya nyavu.

    Bao la Saibari liliweka rekodi mpya: lilikuwa bao la haraka zaidi hadi sasa katika Kombe la Dunia la FIFA 2026, na pia bao la haraka zaidi kuwahi kufungwa na Morocco katika mashindano hayo ya dunia.

    Ushindi huo unaifanya Morocco kufikisha pointi nne na kuongoza Kundi C kabla ya mechi ya Brazil huko Philadelphia.

    Baada ya mapumziko, mchezo uliendelea kuwa wa kasi na mashambulizi ya pande zote mbili. Saibari alikaribia kufunga bao la pili baada ya shuti lake lililopata mguso wa mchezaji wa Scotland kugonga mwamba wa juu, kufuatia Bilal El Khannouss kuvamia upande wa kushoto na kutoa pasi ya chini ndani ya eneo la hatari.

    Morocco ilikaribia tena kufunga muda mfupi baadaye wakati El Khannouss alipokaribia kugeuza kona ya karibu iliyopigwa na Achraf Hakimi kuwa bao, lakini Angus Gunn aliokoa tena kwa ustadi.

    Scotland iliongeza presha katika dakika 15 za mwisho. John McGinn, Ben Doak na Scott McTominay waliongoza mashambulizi mfululizo. Hata hivyo, muda uliisha kabla hawajafanikiwa, na Atlas Lions wakang'ang'ania ushindi muhimu.

    Soma zaidi:

  6. Vifo takriban 30 katika kambi DRC vinaonyesha Ebola inaweza kuwa inaenea kwa kasi

    Watu wasiopungua 30 wamefariki tangu mwanzoni mwa mwezi Mei katika kambi moja ya watu waliokimbia makazi yao kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.

    Maafisa wa kambi walisema kiwango hicho cha vifo hakijawahi kushuhudiwa katika siku za nyuma, kutokana na dalili zilizoripotiwa, kunaweza kuashiria ugonjwa wa Ebola unaosambaa kwa kasi katika eneo hilo.

    Haikuwezekana kuthibitisha chanzo cha vifo hivyo kwa sababu wagonjwa na ndugu zao katika kambi ya Kigonze huko Bunia — kitovu cha mlipuko wa Ebola nchini DRC — walikuwa wamekataa kufanyiwa vipimo ama kwa walio hai au waliokufa, hadi siku ya Alhamisi.

    Hayo yalithibitishwa na msemaji wa kambi pamoja na shirika la misaada la Caritas.

    Hata hivyo, watu wote waliokuwa wamefariki walionyesha dalili kama maumivu ya kichwa, homa na kutapika, ambazo ni dalili zinazohusishwa na Ebola.

    Msemaji wa kambi, baba mmoja aliyempoteza mtoto, vyanzo vitatu vya misaada na kiongozi mmoja wa asasi za kiraia waliliambia shirika la habari la Reuters kuhusu hali hiyo.

    “Hapo kabla watu hawakuwa wakifa kwa namna hii,” alisema msemaji wa kambi, Desire Grodya Bapi, katika mahojiano na Reuters.

    Vifo hivyo katika kambi ya Kigonze, ambayo ina wakazi zaidi ya 15,000, vimezua hofu kwamba Ebola huenda inasambaa bila kugunduliwa miongoni mwa zaidi ya watu milioni 5 waliokimbia makazi yao mashariki mwa Congo.

    Upinzani dhidi ya vipimo pamoja na hali duni ya usafi wa mazingira vinaongeza ugumu wa kudhibiti ugonjwa huo.

    Soma zaidi:

  7. Treni mbili zagongana Uingereza na kusababisha majeraha mabaya

    Dereva wa treni amefariki dunia na watu 89 kujeruhiwa baada ya treni mbili kugongana katika eneo la Bedford.

    Watu 11 walipata majeraha mabaya sana, 22 walijeruhiwa vibaya, na wengine 56 walipata majeraha madogo, kwa mujibu wa Huduma ya Ambulansi ya Mashariki mwa Uingereza.

    Ajali hiyo ilihusisha treni mbili za kampuni ya East Midlands Railway (EMR) zilizokuwa zikielekea kusini kwenda London St Pancras siku ya Ijumaa alasiri. Chanzo cha ajali hiyo bado kinachunguzwa.

    Katibu Mkuu wa chama cha wafanyakazi wa reli cha RMT, Eddie Dempsey, alisema chama hicho “kimehuzunishwa sana kusikia kwamba dereva wa treni na aliyekuwa mwakilishi wa RMT amefariki katika ajali hiyo.”

    Katika taarifa yake, Polisi wa Usafiri wa Uingereza (BTP) walisema wametangaza tukio hilo kuwa dharura kubwa baada ya mgongano huo uliotokea saa 11:15 jioni kwa saa za Uingereza.

    “Tunaelewa kuwa watu kadhaa wamejeruhiwa na kwa masikitiko makubwa mtu mmoja amefariki dunia,” taarifa hiyo ilisema.

    Huduma za treni za East Midlands Railway kwenda na kutoka London St Pancras zilisimamishwa kwa muda wote wa Ijumaa jioni, na usumbufu wa safari unatarajiwa kuendelea hadi Jumamosi.

    Mmoja wa abiria, Dkt. Peter Knapp, aliiambia BBC kwamba alikuwa akisafiri katika behewa la mbele la treni iliyogongana na nyingine.

    “Niliposimama, niliona viti vimetapakaa kila mahali. Ilikuwa ni kana kwamba nilikuwa kwenye mlipuko wa bomu.

    “Niliposimama, niliona nyuso za watu zikiwa zimejaa damu, baadhi ya miguu yao ilionekana kuvunjika, na moshi ulikuwa kila mahali,” alisema.

    Akizungumza akiwa kando ya barabara, Dkt. Knapp alisema polisi walikuwa wakichukua taarifa za abiria huku baadhi yao wakipelekwa hospitalini.

  8. Marekani kusitisha ufadhili wa programu za HIV nchini Afrika Kusini

    Marekani imesema itasitisha ufadhili wa programu nchini Afrika Kusini zilizolenga kupambana na kuenea kwa Virusi vya UKIMWI na Ugonjwa wa UKIMWI.

    Zaidi ya watu milioni nane nchini Afrika Kusini wanaishi na HIV, ikiwa ni idadi kubwa zaidi kuliko nchi yoyote nyingine duniani.

    Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani imeonekana kuhusisha uamuzi huo na madai kwamba Afrika Kusini imeshindwa kulinda jamii ya Waafrika wenye asili ya Kizungu, madai ambayo serikali ya Afrika Kusini imekuwa ikiyakana mara kwa mara.

    Wizara ya Afya ya Afrika Kusini ilijibu kwa kusema kwamba, ingawa haikuwa imefahamishwa rasmi kuhusu uamuzi huo, imekuwa ikifanya kazi kwa muda mrefu kwenye mpango wa kujitegemea kifedha.

    Hadi mwaka 2025, Marekani ilikuwa ikiunga mkono juhudi za Afrika Kusini za kupambana na virusi vya HIV kwa takribani dola milioni 400 za Marekani (£300 milioni) kwa mwaka kupitia Mfuko wa Dharura wa Rais wa Kukabiliana na Ukimwi (PEPFAR).

    Hata hivyo, tangu kuapishwa kwa Donald Trump, uhusiano kati ya nchi hizo mbili umeendelea kuzorota.

    Muda mfupi baada ya kuingia madarakani, Trump alitoa amri ya kiutendaji akidai kwamba sera nyingi za Afrika Kusini zimeondoa usawa wa fursa na kuchochea vurugu dhidi ya wamiliki wa ardhi wanaodaiwa kubaguliwa kwa misingi ya rangi.

    Serikali ya Afrika Kusini inapinga madai hayo na pia imezungumzia uhitaji wa sera yake iliyoanzishwa kurekebisha ukosefu wa usawa wa kiuchumi wa enzi ya ubaguzi wa rangi.

    Soma zaidi:

  9. Mjumbe wa Trump, Waziri wa Iran waelekea Uswizi kwa mazungumzo

    Mjumbe wa Marekani Steve Witkoff na Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araqchi wameelekea Uswisi kwa mazungumzo, shirika la Axios liliripoti siku ya Ijumaa, huku usitishaji wa mapigano nchini Lebanon ukionekana kufufua juhudi za kubadilisha makubaliano ya muda ya kusitisha vita vya Iran kuwa mpango wa kudumu wa kikanda.

    Israel na Hezbollah walikubaliana kusitisha mapigano nchini Lebanon siku ya Ijumaa baada ya kuongezeka kwa mapigano yaliyotia shaka mazungumzo kati ya Marekani na Iran, ambayo ni muhimu kwa ajili ya kufunguliwa tena kwa Mlango-Bahari wa Hormuz na kuleta utulivu wa usambazaji wa mafuta.

    Hatua hiyo ilifuatia hati ya makubaliano yenye vipengele 14 ambayo pande hizo mbili zilitia saini wiki hii ili kusitisha mapigano na kufungua kipindi cha siku 60 cha kutatua mizozo kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran, pamoja na masuala mengine magumu yanayohitajika ili kufikia makubaliano ya kudumu zaidi.

    Hata hivyo, makamu wa Rais wa Marekani JD Vance aliahirisha mipango siku ya Alhamisi ya kusafiri hadi Uswizi kwa mazungumzo hayo, huku kukiwa na mvutano unaoongezeka nchini Lebanon kati ya Israel na Hezbollah, kundi la wanamgambo linaloungwa mkono na Iran.

    Huku usitishaji mapigano ukiwa umeanza kutekelezwa, Witkoff anaelekea Uswizi kuungana na Jared Kushner, mkwe wa Rais Donald Trump, ambaye tayari yuko huko, Axios alisema. Araqchi anapanga kusafiri leo Jumamosi, iliongeza.

    Soma zaidi:

  10. Hujambo na karibu katika matangazo yetu mubashara kwa ajili ya kukujuza kinachotokea katika kila pembe ya dunia. Tarehe ni 20/06/2026, Mimi ni Asha Juma.