Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Trump 'anusurika' katika shambulio la risasi Washington

Kwa mujibu wa maafisa wa usalama, mtu mwenye silaha alivamia hafla ya chakula cha jioni iliyohudhuriwa na Trump na mkewe, na kufyatua risasi kuelekea maafisa wa usalama katika eneo la ukaguzi kabla ya kuingia ukumbini.

Moja kwa moja

Na Yusuph Mazimu

  1. Waziri wa Ulinzi Mali auawa katika shambulio karibu na Bamako

    Waziri wa Ulinzi wa Mali, Sadio Camara, ameripotiwa kuuawa katika shambulio lililolenga makazi yake ndani ya kambi ya kijeshi ya Kati, nje ya mji mkuu Bamako.

    Kwa mujibu wa redio ya Ufaransa RFI, shambulio hilo lilitokea Jumamosi na linahusishwa na kundi la JNIM lenye uhusiano na mtandao wa al-Qaeda. Ripoti hiyo imetolewa leo Jumapili, huku mamlaka za Mali zikiwa bado hazijatoa taarifa rasmi kuhusu tukio hilo.

    Tukio hilo linakuja wakati hali ya usalama nchini Mali ikiendelea kuwa tete, huku makundi ya wenye silaha yakiripotiwa kufanya mashambulizi katika maeneo mbalimbali ya nchi.

  2. Viongozi duniani walivyopokea Trump 'kunusurika' kwenye tukio la risasi Washington

    Baada ya tukio la risasi lililotokea mjini Washington, viongozi mbalimbali wa dunia wametoa ujumbe wa pole, mshikamano na kulaani tukio hilo linaloonekana la kisiasa, huku wakieleza furaha yao kwamba Rais Donald Trump na waliokuwepo walinusurika na wako salama.

    Mark Carney – Waziri Mkuu wa Canada

    Anasema amefarijika kwamba Rais Trump, mke wake, na waliokuwepo wote wako salama. Anaongeza kuwa mawazo yake yako kwa wote waliotikiswa na tukio hilo la kushtua.

    Anthony Albanese – Waziri Mkuu wa Australia

    Anasema amefurahi kusikia kuwa wote waliokuwepo eneo la tukio wako salama. Pia anapongeza kazi ya vyombo vya usalama kwa hatua za haraka.

    Kaja Kallas – Mwakilishi - Umoja wa Ulaya

    Anaonyesha uungaji mkono wake kwa Rais Trump, mkewe na wageni wote, akisisitiza kuwa vurugu za kisiasa hazina nafasi katika demokrasia.

    Delcy Rodríguez – Rais wa mpito wa Venezuela

    Analaani vikali kile alichokiita shambulio lililoshindwa, na anawatakia kila la heri wote waliokuwepo kwenye tukio hilo.

    Shehbaz Sharif – Waziri Mkuu wa Pakistan

    Anasema ameshtushwa sana na tukio hilo, na anatuma maombi yake kwa Rais Trump na wote walioathirika na tukio hilo.

    Narendra Modi – Waziri Mkuu wa India

    Anatuma salamu za heri na kuwatakia usalama na afya njema Rais, mkewe na Makamu wa Rais.

    Claudia Sheinbaum – Rais wa Mexico

    Anasema “tunatoa heshima zetu,” akisisitiza kuwa vurugu hazipaswi kuwa njia ya kutatua tofauti katika jamii yoyote.

  3. Mwanzo mwisho kuhusu tukio la risasi Washington ilivyotokea

    Hapa chini ni muhtasari wa namna tukio la risasi lililoripotiwa katika Hoteli ya Washington Hilton, Marekani lilivyotokea, ukionyesha muda kwa saa za Afrika Mashariki (EAT) na kwenye mabano kwa saa za Mashariki ya Marekani (ET – Eastern Time. Rais Donald Trump, mkewe na viongozi wengine wa Marekani akiwemo Makamu wa rais, JD Vance. walinusurikia kwa kuondolewa na walinzi haraka.

    Lilitokea alfajiri kuanzia saa 03:35 kwa saa za Afrika Mashariki ambayo ilikuwa saa 20:35 usiku kwa saa za Washington D.C., Marekani).

    03:35 EAT (20:35 ET – Washington D.C., Marekani) Milio ya risasi inasikika katika Hoteli ya Washington Hilton iliyopo Washington D.C. Wageni wanajificha kchini ya meza wa hofu. Maafisa wa usalama wanamfikia haraka Donald Trump na watu wake wa karibu na kuwatoa eneo la tukio kwa ulinzi mkali.

    04:17 EAT (21:17 ET – Washington D.C., Marekani) Donald Trump anatoa taarifa yake ya kwanza kupitia mtandao wa Truth Social, akisema mshukiwa wa tukio hilo “amekamatwa”.

    04:36 EAT (21:36 ET – Washington D.C., Marekani) Trump anasema anaondoka katika hoteli hiyo kwa maelekezo ya vyombo vya usalama na sheria.

    05:29 EAT (22:29 ET – Washington D.C., Marekani) Trump anachapisha video inayoonekana kuonyesha mwanzo wa tukio la risasi. Baadaye anachapisha pia picha ya mshukiwa.

    05:30 EAT (22:30 ET – Washington D.C., Marekani) Anazungumza katika mkutano na waandishi wa habari akiwa Ikulu ya White House, akiwa na maafisa wakuu wa serikali. Anasema kuna uwezekano mshukiwa alikuwa akifanya kazi peke yake (“lone wolf”).

    05:50 EAT (takriban 22:50 ET – Marekani) Vyombo vya habari vya Marekani, ikiwemo CBS, vinamtaja mshukiwa kuwa ni Cole Tomas Allen, mwenye umri wa miaka 31, kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya uchunguzi.

    06:10 EAT (takriban 23:10 ET – Torrance, California, Marekani) Picha za moja kwa moja zinaonyesha polisi wakifanya msako katika nyumba moja mjini Torrance, California, kama sehemu ya uchunguzi unaoendelea.

    06:15 EAT (takriban 23:15 ET – Washington D.C., Marekani) Mwanasheria wa Marekani wa huko eneo la Columbia anasema mshukiwa anatarajiwa kufikishwa mahakamani Jumatatu kwa mashtaka rasmi.

  4. Tanzania yasema hakuna uthibitisho wa watanzania kushambuliwa Afrika Kusini

    Serikali ya Tanzania imesema hadi sasa hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha Mtanzania amehusika au ameathirika katika matukio ya mashambulizi yanayoripotiwa kuwalenga raia wa kigeni nchini Afrika Kusini.

    Akizungumza kuhusu taarifa hizo zinazosambaa mitandaoni, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, amesema video zinazotumika kuhusisha matukio hayo zimebainika kuwa ni za zamani na si za sasa.

    “Mpaka sasa hakuna uthibitisho wa Mtanzania kushambuliwa. Video zinazosambazwa tumebaini ni video za zamani,” amesema Msigwa.

    Msigwa ameongeza kuwa serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu hali inayoendelea Afrika Kusini na inatoa wito kwa mtu yeyote mwenye taarifa au uthibitisho wa Mtanzania aliyeathirika kutoa taarifa katika ubalozi wa Tanzania nchini humo.

    Kumekuwa na wimbi la waafrika kukimbilia afrika kusini kutafuta maisha, wengi wakiingia bila kufuata utaratibu na kukumbana na mashambulizi ya wenyeji.

    Katika kipindi cha Januari hadi Disemba, 2025, takribani Watanzania 450 walikamatwa Afrika Kusini na kurejeshwa nchini baada ya kubainika waliingia bila kufuata taratibu sahihi za uhamiaji.

  5. Aliponusurika Trump ndipo alipojeruhiwa kwa risasi Rais Reagan mwaka 1981

    Tukio la leo la shambulio la risasi limetokea katika Hoteli ya Washington Hilton iliyopo Connecticut Avenue, eneo lilelile ambalo Rais wa zamani wa Marekani Ronald Reagan alipigwa risasi na kujeruhiwa mwaka 1981.

    Shambulio hilo lilitokea tarehe 30 Machi 1981, wakati mshambuliaji John Hinckley Jr alipofyatua risasi dhidi ya Reagan alipokuwa akirejea kwenye gari lake la rais baada ya kutoa hotuba ndani ya hoteli hiyo.

    Reagan alinusurika lakini alijeruhiwa vibaya baada ya risasi kupiga gari lake la rais na kumpiga tumboni, ikimvunja ubavu na kutoboa pafu moja. Alikimbizwa katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha George Washington iliyo karibu, na baadaye aliruhusiwa kutoka hospitalini tarehe 11 Aprili, karibu wiki moja na nusu baadaye.

    Mwaka uliofuata, Hinckley alipatikana hana hatia kwa sababu ya alibainikwa kuwa na ugonjwa wa akili, lakini alishikiliwa katika sehemu yenye ulinzi wa hali ya juu katika Hospitali ya St. Elizabeths mjini Washington hadi alipoachiliwa mwaka 2016, miaka 35 baadaye.

    Mpaka leo bado kuna kibao cha kumbukumbu kinachoonyesha eneo la tukio hilo upande wa hoteli hiyo.

  6. Picha mbali mbali za tukio la risasi Washington

  7. Mshukiwa wa tukio la risasi Washington atambuliwa na atafikishwa Mahakamani kesho

    Mamlaka za Marekani zimetambua mshukiwa wa tukio hilo kuwa ni Cole Tomas Allen, mwenye umri wa miaka 31 kutoka Torrance, California. Anatarajiwa kufikishwa mahakamani Jumatatu kujibu mashtaka yake.

    Mwanasheria wa kutoka eneo la Columbia, Marekani, Jeanine Pirro, amesema anakabiliwa na makosa ya kutumia silaha katika uhalifu wa vurugu pamoja na kushambulia maafisa wa serikali kwa kutumia silaha hatari.

    Amesema kesi hiyo itasikilizwa katika mahakama ya shirikisho, na hatua za kisheria tayari zimeanza kuchukuliwa dhidi yake.

    Polisi wamesema bado wanachunguza chanzo cha tukio hilo, lakini mshukiwa alikamatwa eneo la ukaguzi lililowekwa kwa usalama wa hafla hiyo.

  8. Mshukiwa wa tukio la risasi Washington alikuwa mgeni wa hoteli, polisi wasema

    Polisi wa Washington DC wamesema mshukiwa wa tukio la kufyatua risasi katika hafla ya Waandishi wa Habari wa Ikulu Marekani, alikuwa mgeni katika hoteli iliyokuwa mwenyeji wa hafla hiyo.

    Kiongozi mwandamizi wa Polisi, Jeff Carroll, amesema chumba chake kimeshikiliwa kama sehemu ya uchunguzi unaoendelea.

    Amesema mshukiwa huyo hakuwahi kujulikana na polisi kabla ya tukio hilo, na hakuna ishara ya awali iliyokuwa ikionyesha hatari yoyote.

    Polisi pia wamesema eneo la ukaguzi lililopo kwenye mlango wa tukio hilo lilisaidia kumkamata mshukiwa haraka mara baada ya tukio.

    Aidha, mamlaka zimesema kwa sasa hakuna dalili za kuwepo kwa tishio lingine kwa umma.

  9. Risasi zasikika Washington, Trump aokolewa na walinzi

    Rais Donald Trump na mkewe Melania Trump waliondolewa haraka kwenye hafla ya kila mwaka ya chakula cha jioni ya waandishi wa habari (White House Correspondents’ Dinner) mjini Washington DC baada ya mtu mwenye silaha kuvamia na kufyatua risasi karibu na eneo la usalama.

    Kwa mujibu wa maafisa wa usalama, mshukiwa huyo alifyatua risasi kuelekea maafisa wa usalama katika eneo la ukaguzi kabla ya kuingia ukumbini. Afisa mmoja alipigwa risasi lakini hakupata madhara makubwa kutokana na kuvaa kuizuia risasi na hali yake inaelezwa kuwa nzuri.

    Washiriki wa hafla hiyo, wakiwemo viongozi wa serikali na wanahabari, walilazimika kujificha chini ya meza huku vikosi vya usalama vikichukua hatua za haraka kumdhibiti mshukiwa huyo.

    Mshukiwa huyo, aliyekuwa na silaha kadhaa, alikamatwa na mamlaka na anaaminika kuwa alitenda tukio hilo akiwa peke yake. Hakuna viongozi wa serikali walioumia katika tukio hilo.

    Baada ya tukio hilo, Trump aliwashukuru maafisa wa usalama kwa hatua zao za haraka na kusema tukio hilo linachunguzwa zaidi huku sababu za mshambulizi bado hazijajulikana.

    Hafla hiyo, iliyokuwa imehudhuriwa na mamia ya watu wakiwemo viongozi wakuu wa serikali, ilisitishwa kufuatia tukio hilo la ghafla la kiusalama.

  10. Karibu katika habari zetu za moja kwa moja leo Jumapili Aprili 26, 2025