Uingereza yashinda kesi kuhusu mkataba wa wahamiaji wa Rwanda uliovunjika
Mahakama imeamua Uingereza haitailipa Rwanda mamilioni ya pauni kufuatia kusitishwa kwa mkataba wa wahamiaji.
Mahakama ya kimataifa imeamua kwamba Uingereza haitalazimika kuilipa Rwanda mamilioni ya pauni kufuatia kusitishwa kwa makubaliano ya kuwahamishia waomba hifadhi nchini Rwanda, mpango uliositishwa na Waziri Mkuu wa Uingereza, Keir Starmer, muda mfupi baada ya kuingia madarakani.
Serikali ya Rwanda ilikuwa imewasilisha madai ya zaidi ya pauni milioni 100 dhidi ya Uingereza, ikidai kuwa ilikiuka masharti ya makubaliano hayo.
Makubaliano hayo, yaliyosainiwa na serikali ya awali ya Chama cha Conservative, yalilenga kuifanya Rwanda iwe mwenyeji wa waomba hifadhi waliowasili Uingereza kwa njia zisizo halali, huku Uingereza ikigharamia mpango huo.
Katika usikilizwaji wa kesi uliofanyika kwa siku tatu nchini Uholanzi, mawakili wa Uingereza walieleza kuwa ilikuwa jambo la kawaida kabisa kwa mpango huo kufutwa baada ya chama cha Labour kuingia madarakani, na kwamba hakukuwa na sababu ya kufanya malipo zaidi baada ya kusitishwa kwa mpango huo.
Pia walikanusha madai kwamba Uingereza ilikiuka sehemu yoyote ya makubaliano hayo.
Wakili wa Uingereza aliiambia mahakama mjini The Hague kwamba Rwanda haikuwa na haki ya kupata fidia yoyote iliyokuwa ikiidai.
Kwa upande mwingine, Waziri wa Sheria na Mwanasheria Mkuu wa Rwanda, Emmanuel Ugirashebuja, aliieleza mahakama kuwa Rwanda ilikuwa tayari imetumia fedha nyingi kujiandaa kwa utekelezaji wa ushirikiano huo, lakini Uingereza ilijiondoa katika wajibu wake wa kisheria.
Pia alisema kuwa Uingereza haikuipa Rwanda taarifa ya awali kuhusu uamuzi wa kusitisha makubaliano hayo, na kwamba viongozi wa Rwanda walilazimika kupata habari hiyo kupitia vyombo vya habari.
Uamuzi huo wa mahakama unaondoa madai ya fidia ambayo Rwanda ilikuwa ikitaka kutoka Uingereza kutokana na kusitishwa kwa mpango huo wa wahamiaji.
Unaweza kusoma;