Aliyekuwa kiongozi wa genge la Crips apatikana na hatia ya mauaji ya Tupac Shakur
Aliyekuwa kiongozi wa genge la uhalifu, Duane "Keffe D" Davis, amepatikana na hatia ya kupanga mauaji ya Tupac Shakur – hii ikiwa ni hukumu ya kwanza katika kesi ya muda mrefu ambayo haikutatuliwa na iliyowavutia mashabiki wa muziki wa hip-hop kwa karibu miaka 30.
Baraza la wazee wa mahakama lilimkuta Davis na hatia ya shtaka moja la mauaji kwa kutumia silaha hatari kuhusiana na kifo cha nyota huyo wa rap, aliyeuawa kwa kupigwa risasi kutoka kwenye gari linaloenda kasi jijini Las Vegas mnamo tarehe 7 Septemba 1996.
Akiwa amevaa suti nyeusi, mwanamume huyo mwenye umri wa miaka 63 alisimama bila kuonyesha hisia zozote mahakamani huko Las Vegas wakati hukumu ikisomwa, kabla ya kusema kuwa atakata rufaa.
Jamaa wa Shakur walishikana mikono, huku baadhi yao wakikumbatiana na kulia.
Shakur alikuwa na umri wa miaka 25 alipouawa akiwa katika kilele cha taaluma yake kama mmoja wa wasanii wenye ushawishi mkubwa katika muziki wa rap.
Amefanikiwa kuuza zaidi ya rekodi milioni 75 duniani kote.