Haiti kufanya uchaguzi wa kwanza baada ya muongo mmoja
Baraza la uchaguzi la Haiti (CEP) limetangaza Jumatatu kuwa uchaguzi wa kwanza wa urais baada ya miaka kumi utafanyika mnamo mwezi Desemba, huku duru ya pili ya uchaguzi ikipangwa kufanyika mwezi Februari.
Awali, uchaguzi huo ulipangwa kufanyika mwezi Agosti na duru ya pili mwezi Desemba, lakini uliahirishwa kutokana na wasiwasi kuhusu hali ya usalama.
Haiti haijafanya uchaguzi tangu mwaka 2016.
Rais wake wa mwisho, Jovenel Moise, aliuawa mwaka 2021 baada ya kuchelewesha kufanyika kwa uchaguzi. Serikali zilizofuata zilipewa jukumu la kuandaa uchaguzi, lakini zilisema hali ya ukosefu wa usalama kutokana na mapigano na magenge yenye silaha yenye nguvu imefanya hilo lisiwezekane.
Siku ya Jumatatu, baraza hilo la uchaguzi lilitoa ratiba inayoonyesha kuwa awamu ya kwanza ya uchaguzi wa rais na wabunge nchini Haiti itafanyika tarehe 13 Desemba, huku duru ya pili ya uchaguzi ikifanyika tarehe 21 Februari. Pia limetangaza kuwa matokeo ya mwisho yatachapishwa tarehe 7 Machi.
Wananchi pia wanatarajiwa kupiga kura kuhusu mabadiliko ya katiba pamoja na kuwachagua viongozi wa maeneo ya serikali za mitaa, kulingana na ratiba hiyo.
Baraza hilo lilisisitiza kuwa utekelezaji wa ratiba hiyo unategemea "kuwepo kwa hali ya usalama inayokubalika na kupatikana kwa fedha zinazohitajika kuendesha shughuli za uchaguzi."
Mapema mwezi huu, baraza hilo lilisema limeanza kusajili wapiga kura na kutoa mafunzo kwa maafisa wa usalama wa uchaguzi. Pia lilichapisha orodha rasmi ya zaidi ya vyama 300 vya kisiasa vilivyoidhinishwa kushiriki katika mchakato wa uchaguzi unaokuja.
Pia Unaweza Hapa: